1
HOTUBA YA MHESHIMIWA DR. JAKAYA MRISHO
KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA
TANZANIA WAKATI WA KUAGANA NA BUNGE NA
KULIVUNJA BUNGE LA KUMI LA JAMHURI YA
MUUNGANO WA TANZANIA, UKUMBI WA BUNGE,
DODOMA TAREHE 9 JULAI, 2015
Mheshimiwa Spika;
Tunayo kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu
mwingi wa rehma kwa kutujalia uzima na kutuwezesha
kuishuhudia siku hii adhimu katika historia ya Bunge letu
na nchi yetu. Hatimaye siku ya kuvunja Bunge la Kumi
imewadia ili kuwezesha hatua husika za mchakato wa
Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ziweze kutekelezwa.
Nakushukuru sana Mheshimiwa Spika kwa kunipatia
nafasi hii ya kulihutubia Bunge lako tukufu ili niweze
kutimiza wajibu wangu huo wa msingi Kikatiba. Lakini,
shukrani zangu kubwa ni kwa uongozi wako mahiri na
shupavu. Umeliongoza Bunge vizuri. Najua haikuwa kazi
rahisi. Penye wengi pana mengi. Lakini kwa uhodari
2
mkubwa umeweza kulifikisha jahazi bandarini salama
salmini. Hakika wewe ni nahodha makini na jemedari
hodari, uliyethibitisha uhodari na umakini wako katika
uwanja wa medani. Wewe ndiwe mwanamke wa kwanza
kushika wadhifa huu wa juu kabisa katika mhimili huu wa
kutunga sheria na umeidhihirishia dunia kuwa wanawake
wakipewa nafasi wanaweza.
Mheshimiwa Spika;
Niruhusu pia nitoe shukrani na pongezi zangu za dhati
kwa Waheshimiwa Wabunge kwa kazi kubwa na nzuri
mliyoifanya. Mmetimiza ipasavyo wajibu wao wa Kikatiba
wa Kutunga Sheria na kusimamia Serikali. Nawashukuru
kwa ushirikiano wenu na msaada wenu. Ni ukweli ulio
wazi kuwa bila ya ninyi Wabunge wetu na Bunge hili,
tusingeweza kupata mafaniko na maendeleo tuliyoyapata.
Mmejijengea, nyinyi wenyewe na Bunge letu heshima
kubwa mbele ya wananchi. Mmeitendea haki demokrasia
3
ya Tanzania na kuliletea heshima kubwa Bunge letu nchini,
kikanda na kimataifa.
Mheshimiwa Spika;
Tarehe 30 Desemba 2005 nilipozindua Bunge la Tisa
nilielezea mtazamo wangu kuhusu nchi yetu na kutaja
majukumu ya msingi na vipaumbele vya Serikali ya Awamu
ya Nne. Nilisema tutatekeleza wajibu wetu na vipaumbele
hivyo kwa ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya. Tarehe 16
Julai, 2010 wakati wa kuvunja Bunge hilo nilielezea
mafanikio tuliyopata na changamoto zilizotukabili katika
kipindi hicho. Tarehe 28 Novemba, 2010 wakati wa
kuzindua Bunge hili la Kumi niliainisha vipaumbele vya
Serikali ya Chama cha Mapinduzi katika kipindi changu cha
pili cha uongozi wa nchi yetu na kuahidi kuvitekeleza kwa
ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaidi. Kama ilivyo ada, leo
tunafikia mwisho wa uhai wa Bunge la Kumi, naomba
kutumia fursa hii kutoa mrejesho wa utekelezaji wa
4
majukumu ya Serikali na yale mambo ambayo tuliahidi na
kupanga kufanya.
Umoja, Amani na Usalama
Mheshimiwa Spika;
Niliahidi kuwa katika kipindi cha uongozi wangu
nitafanya kila niwezalo kuhakikisha kuwa Tanzania
inaendelea kuwa nchi moja na watu wake wanaendelea
kuwa wamoja, wanaopendana na kushirikiana licha ya
tofauti zao za rangi, dini, makabila, mahali watokako, na
ufuasi wa vyama vya siasa. Pia, kwamba nchi yetu
itaendelea kuwa yenye amani, usalama na utulivu.
Leo tunapoagana, ninyi na mimi, ni mashuhuda kuwa
Tanzania na Watanzania tumebakia kuwa wamoja. Hata
hivyo, katika kipindi hiki kumekuwepo na matukio ya hapa
na pale madogo na makubwa, yaliyotishia umoja wa nchi
yetu na watu wake. Yapo mambo yaliyopandikizwa kuleta
chuki baina ya Tanzania Bara na Zanzibar, baina ya
5
Wakristo na Waislamu na baina ya maeneo fulani ya nchi na
wengine.
Bahati nzuri, msimamo thabiti wa viongozi wakuu wa
Serikali zetu mbili wakisaidiwa na viongozi wengine pamoja
na ushirikiano na viongozi wa dini na wa jamii na uelewa
wa wananchi, vimeliwezesha taifa letu kushinda
changamoto hizo na matishio yote hayo. Changamoto hizi
zimethibitisha ubora wa mazungumzo. Ni kweli kabisa
kwamba wanaozungumza hawagombani na
wanaozungumza humaliza tofauti zao bila kugombana.
Mheshimiwa Spika;
Niruhusuni, nitumie nafasi hii kuwashukuru kwa mara
nyingine viongozi wakuu wenzangu, Makamu wa Rais, Rais
wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Waziri Mkuu, Makamu
wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Makamu wa Pili wa Rais
Zanzibar, viongozi wa dini, viongozi wa jamii na wananchi
wote kwa ushindi tulioupata katika kudumisha umoja wetu.
Hata hivyo, tahadhari kubwa lazima iendelee kuchukuliwa
6
kwani watu wenye nia mbaya kwa nchi yetu au na umoja
wetu hawajaisha na hawajafurahi kwamba hawajafaulu.
Huenda wakajaribu tena. Tunachotakiwa kufanya ni
kuendelea kushikamana ili hata wakijaribu tena washindwe.
Muungano Wetu Umeimarika Zaidi
Mheshimiwa Spika;
Nafurahi kwamba namaliza kipindi changu cha
uongozi tukiwa tumeweza kudumisha na kuuimarisha
Muungano wetu adhimu na adimu Barani Afrika.
Mtakumbuka kuwa katika hotuba yangu ya kufungua
Bunge la Tisa nilisisitiza umuhimu wa viongozi wa pande
zetu mbili kukutana mara kwa mara kuzungumzia ustawi
wa Muungano wetu. Nafurahi kwamba jambo hili
limefanyika chini ya uenyekiti wa Makamu wa Rais,
akisaidiwa na Waziri Mkuu kwa upande wa Tanzania Bara
na kwa upande wa Zanzibar, Waziri Kiongozi katika awamu
yangu ya kwanza na Makamu wa Pili wa Rais katika
awamu hii.
7
Mafanikio yaliyopatikana ni makubwa. Masuala
mbalimbali ya zamani na mapya yamezungumzwa,
yameshughulikiwa na kupatiwa ufumbuzi. Kwa mfano,
hadi mwaka 2005 zilikuwa zimebakia kero 13 za Muungano
zilizoainishwa na Tume ya Shelukindo, hivi sasa zimebaki
kero nne. Tayari ufumbuzi wa kero moja unakamilishwa
kiutawala na tatu zimeshughulikiwa kwa ukamilifu katika
Katiba Inayopendekezwa. Kama kura ya maoni ingekuwa
imefanyika na Katiba hiyo kupitishwa kungekuwa hakuna
kiporo cha kero za Tume ya Shelukindo. Lakini kwa vile
kura ya maoni haijafanyika ndiyo maana tunaendelea
kuzitaja. Hata hivyo, Serikali zetu mbili zimezungumza na
kukubaliana tutafute njia ya kumaliza suala la rasilimali ya
mafuta na gesi. Ndiyo maana katika Muswada wa Petroli
hoja ya Zanzibar kuwa na mamlaka kamili ya kusimamia
uchimbaji wa mafuta na kumiliki mapato yake ilijumuishwa.
Natoa shukrani nyingi kwa Bunge lako tukufu kwa
8
kupitisha Muswada huo. Moja ya kero kubwa katika
Muungano tumeimaliza.
Mpasuko wa Kisiasa Zanzibar
Mheshimiwa Spika;
Mtakumbuka kuwa nilizungumzia kusononeshwa
kwangu na mpasuko wa kisiasa uliokuwepo Zanzibar
wakati ule na kuelezea utayari wangu wa kusaidia
kuuondoa. Kama mjuavyo mazungumzo yalifanyika ndani
ya CCM na CUF na baina ya vyama hivyo na muafaka
ukapatikana. Serikali ya Umoja wa Kitaifa ikaundwa na
mpasuko wa kisiasa ukawa umepatiwa tiba. Matokeo ya
yote hayo ni kuwa mazingira ya kisiasa na kijamii
yamekuwa bora zaidi siku hizi kuliko ilivyokuwa kabla ya
hapo.
Ni matumaini yangu kuwa ndugu zetu wa Zanzibar
watayadumisha mafanikio haya ili waendelee kuishi kwa
9
amani, upendo na udugu. Natambua kuwepo kwa
changamoto za hapa na pale katika uendeshaji wa Serikali
hiyo. Jambo linalonipa faraja ni kuwa matatizo yenyewe
hayahusu muundo wa Serikali bali yanaletwa na watu
kupishana kauli au kutofautiana katika uendeshaji wa
baadhi ya mambo. Mimi naamini hayo ni mambo
yanayoweza kumalizwa kwa wadau kukaa kitako na
kuzungumza kama ilivyokuwa kabla ya muafaka.
Amani na Usalama
Mheshimiwa Spika;
Nchi yetu iko salama, mipaka iko salama kwa sababu
Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania limeendelea
kutimiza ipasavyo jukumu lake la kulinda uhuru na mipaka
ya nchi yetu. Katika kipindi hiki tumewekeza sana katika
kuliimarisha Jeshi letu kwa vifaa na zana za kisasa za kivita
na mafunzo. Tumeimarisha Kamandi za Nchi Kavu, Anga
na Majini. Utayari kivita wa jeshi letu ni mzuri tena wa hali
ya juu. Weledi na nidhamu ya Wanajeshi wetu ni ya hali ya
10
juu. Tumeboresha maslahi na makazi ya wanajeshi kwa
kujenga nyumba mpya za kuishi. Utekelezaji wa mpango wa
kuwajengea nyumba 10,000 unaendelea vizuri. Hadi hivi
sasa nyumba 6,064 zinaendelea kujengwa nchi nzima na kati
yake nyumba 3,096 zimekamilika. Namaliza kipindi changu
cha kuwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na
Usalama kwa kujiamini kwamba Tupo vizuri. Pamoja na
hayo kazi ya utekelezaji wa Mpango wa Miaka 15 wa
kuimarisha JWTZ lazima iendelezwe ili kulifikisha Jeshi letu
pale tulipopakusudia.
Mheshimiwa Spika;
Katika miaka 10 hii tumefanya jitihada kubwa ya
kupambana na uhalifu ili kulinda usalama wa maisha na
mali za watu waishio Tanzania. Mtakumbuka kuwa mwaka
2005 na mwanzoni mwa 2006 kulikuwa na matukio mengi
ya ujambazi. Niliahidi wakati wa kampeni na katika hotuba
yangu Bungeni kwamba hatutawaacha majambazi
waendelee kutamba. Hali ile imedhibitiwa. Ingawaje
11
matukio ya ujambazi hayajaisha, lakini hayako kama
ilivyokuwa wakati ule.
Hali kadhalika, matukio ya uhalifu wa kuwania mali
yamepungua kutoka 53,268 mwaka 2005 hadi 43,808 mwaka
2014. Natoa pongezi nyingi kwa Jeshi la Polisi kwa kazi
kubwa na nzuri waliyoifanya na wanayoendelea kufanya.
Jambo ambalo bado hatujafanikiwa vya kutosha ni ajali za
barabarani. Lazima tuendelee kuzitafutia muarobaini wake.
Niruhusuni niwatambue na kuwashukuru Inspekta Jenerali
(mstaafu) Omari Mahita, Inspekta Jenerali (mstaafu) Said
Mwema na Inspekta Jenerali Ernest Mangu aliyepo sasa kwa
uongozi wao mzuri.
Mafanikio haya ni matokeo ya uwekezaji wa Serikali
katika utakelezaji wa mpango wa maboresho ya Jeshi la
Polisi uliobuniwa wakati wa uongozi wa Ndugu Saidi
Mwema, IGP mstaafu. Jeshi la Polisi linaendelea
kuwezeshwa kwa zana, vifaa na mafunzo. Taratibu
12
zimekamilika za kulipatia Jeshi hilo magari ya kutosha ili
kuongeza ufanisi.
Pia, tumeendelea kuboresha maslahi na mazingira ya
kuishi Maafisa na Askari. Kwa ajili hiyo tumekarabati
baadhi ya nyumba zilizopo, tumejenga nyumba kadhaa
mpya za ghorofa, za kawaida na mabweni. Mipango
imekamilika ya kuwezesha ujenzi wa nyumba 10,000
ambazo zitapunguza kwa kiasi kikubwa tatizo la uhaba wa
nyumba za kuishi katika Jeshi la Polisi.
Mheshimiwa Spika;
Jeshi letu la Magereza nalo limeendelea kutekeleza
vizuri majukumu yake ya kulinda wafungwa na
kurekebisha tabia zao. Aidha, huduma za malazi, mavazi,
chakula na usafiri kwa wafungwa zimeendelea kuboreshwa.
Changamoto kubwa ni msongamano wa wafungwa
Magerezani. Naamini mipango ya kujenga magereza mapya
na kupanua yaliyopo ikitekelezwa tatizo litaisha. Aidha,
mpango wa maboresho ya Jeshi la Magereza ukikamilika na
13
kutekelezwa, utaboresha mazingira ya kufanyia kazi na
kuishi maafisa na askari, hivyo kupandisha morali wao na
kuongeza ufanisi.
Jeshi la Kujenga Taifa
Mheshimiwa Spika;
Ahadi yangu ya kuanzisha upya utaratibu wa
kuchukua vijana wa mujibu wa Sheria katika Jeshi la
Kujenga Taifa imetimia. Mpaka hivi sasa vijana 38,200
wamekwisha hitimu mafunzo hayo wakiwemo
Waheshimiwa Wabunge. Nawapongeza sana Waheshimiwa
Wabunge walioshiriki kwa kuongoza kwa mfano. Imesaidia
sana utaratibu huo kuanza upya bila vipingamizi. Ni
matumaini yangu kuwa Wizara ya Fedha, Wizara ya Ulinzi
na Jeshi la Kujenga Taifa watakaa pamoja kujadili namna ya
kutafuta ufumbuzi kwa changamoto zilizopo. Naamini
zinaweza kumalizwa, vijana wetu wakashiriki mafunzo bila
matatizo yoyote.
14
Utawala Bora
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi cha miaka kumi hii tumetekeleza
dhamira yetu ya kujenga na kuimarisha utawala bora kwa
sera, sheria, mifumo, taasisi na kwa rasilimali watu.
Tumefanya hivyo katika maeneo yote muhimu yakiwemo
yale yahusuyo haki za binadamu, demokrasia, mapambano
dhidi ya rushwa, maadili ya viongozi, ukusanyaji wa
mapato na nidhamu ya matumizi ya fedha za umma na
mgawano wa madaraka hati ya mihimili.
Bunge la Jamhuri ya Muungano
Mheshimiwa Spika;
Serikali imetimiza ipasavyo wajibu wake kwa mhimili
mkuu wa dola wa Kutunga Sheria. Tulianzisha Mfuko wa
Bunge na kuongeza fedha katika bajeti ya Bunge toka
shilingi bilioni 30.58 mwaka 2005/06 hadi shilingi bilioni
173.76 mwaka 2015/16. Pia tumeanzisha Mfuko wa Jimbo ili
15
kuwawezesheni Wabunge kuchangia katika kutatua
changamoto za maendeleo zinazowakabili wananchi wa
majimbo yao. Bunge letu limetekeleza ipasavyo majukumu
yake kupitia Kamati zake za kudumu na pale ilipolazimu
Kamati teule zilizoundwa.
Katika kipindi hiki miswada 163 imepitishwa, maswali
ya msingi 7,544 na ya nyongeza 22,632 yameulizwa na
kujibiwa. Kamati teule 2 ziliundwa. Haya ni mafanikio
makubwa kwa Bunge letu. Bunge hili limefanya kazi kubwa
na kazi ya kutukuka. Michango na ushauri wake umekuwa
chachu ya baadhi ya hatua na mabadiliko ya kisera, kisheria
na kiutendaji yaliyofanywa na Serikali. Kwa kweli
mnastahili pongezi nyingi. Huwezi kutaja mafanikio ya
Serikali ya Awamu ya Nne bila kutambua mchango wa
Bunge hili.
Mchakato wa Katiba
Mheshimiwa Spika;
16
Kama sote tujuavyo, kupitia Sheria iliyotungwa na
Bunge hili, mwaka 2013 tulianzisha mchakato wa
Mabadiliko ya Katiba kwa lengo la kuipatia nchi yetu Katiba
mpya iliyo bora zaidi kuliko iliyopo sasa. Nafurahi kwamba
mchakato huo ulituwezesha kupata Katiba
Inayopendekezwa ambayo imekidhi matarajio hayo.
Narudia kutoa pongezi za dhati kwa Tume ya Mabadiliko
ya Katiba na Bunge Maalum la Katiba kwa kazi kubwa na
nzuri waliyofanya. Hatua iliyobaki ni Kura ya Maoni
ambapo sote tunasubiri maelekezo ya Tume ya Uchaguzi.
Mimi naamini iwapo itapitishwa, Katiba Inayopendekezwa
itaimarisha zaidi taifa letu.
Vyama vya Siasa
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki tumeshuhudia vyama vya siasa
vikiendelea kuimarika na kujijenga nchini. Idadi ya vyama
vya siasa imeongezeka kutoka 18 hadi 24. Vyama vya siasa
vimefanya shughuli zake kwa uhuru. Viongozi na
17
wanachama wao wamefanya mikutano mingi na hata
maandamano kote nchini. Baraza la Vyama vya Siasa na
TCD vimekuwa vyombo muhimu vilivyofanya kazi nzuri ya
kujenga ushirikiano miongoni mwa vyama vya siasa.
Yamekuwa majukwaa muhimu ya mashauriano baina ya
vyama vya siasa kwa masuala mbalimbali. Matatizo na
changamoto nyingi zimeweza kupatiwa ufumbuzi. Ni
matumaini yangu kuwa vyombo hivi viwili vitaendelezwa
na kuimarishwa miaka ijayo.
Huu ni mwaka wa Uchaguzi, na vyama vya siasa ndiyo
wahusika wakuu. Ni matumaini yangu kuwa vyama vya
siasa vitaheshimu na kuzingatia maadili ya uchaguzi. Hii
itasaidia kuwepo kwa utulivu na amani katika mchakato wa
uchaguzi.
Uchaguzi Mkuu
Mheshimiwa Spika;
Habari kubwa hapa nchini sasa ni uchaguzi mkuu.
Tayari Tume ya Uchaguzi ya Taifa (NEC) na ile ya Zanzibar
18
(ZEC) zimekwisha tangaza tarehe 25 Oktoba, 2015 kuwa ni
siku ya kufanyika uchaguzi mkuu. Maandalizi ya uchaguzi
huo yanaendelea vizuri. Tume ya Taifa ya Uchaguzi
inaendelea na zoezi la uandikishaji wa wapiga kura kwa
mfumo mpya wa teknolojia ya Biometric Voters Register
(BVR). Hadi sasa zoezi la uandikishaji limekamilika katika
mikoa 13 na linaendelea katika mikoa 11 na katika mkoa wa
Dar es Salaam na Zanzibar uandikishaji unategemea kuanza
mwezi huu. Kwa taarifa za Tume ya Uchaguzi, tayari
wamekwisha andikisha hadi sasa wapiga kura milioni 11
kati ya lengo la kuandikisha wapiga kura kati ya milioni 21
hadi 23.
Sisi katika Serikali tutaendelea kutimiza wajibu wetu
wa kuiwezesha Tume kutimiza wajibu wake. Napenda
kuwahakikishia kuwa kila Mtanzania mwenye haki ya
kupiga kura atapata fursa ya kuandikishwa. Shime
tuhimize watu wajitokeze kujiandikisha ili wasikose haki
yao hiyo.
19
Uhuru wa Habari
Mheshimiwa Spika;
Mtakubaliana nami kuwa katika kipindi hiki uhuru wa
habari na uhuru wa watu kutoa maoni yao umepanuka
sana. Tanzania kuna magazeti ya kila siku 16 na kati ya hayo
ya Serikali ni 2 (Daily News, Habari Leo). Pia magazeti ya
kila wiki yapo 62. Aidha, kuna vituo vya redio 115 na vya
televisheni 29. Serikali haifanyi uhakiki wa habari kabla ya
kuchapishwa au kuandikwa. Tumeamua hivyo kwa imani
yangu kwamba ustawi wa demokrasia hutegemea sana
uhuru wa vyombo vya habari. Pili, kwa vile tunatambua
manufaa ya vyombo vya habari kuelimisha jamii,
kupambana na maovu na kuhimiza uwajibikaji.
Pamoja na hayo, hatukusita wala kuchelea kuchukua
hatua pale uhuru huo ulipotumiwa vibaya na kutishia
kuvuruga amani, umoja na usalama wa jamii au taifa. Au,
20
pale ambapo Sheria za nchi zimekiukwa. Huo ni wajibu
wetu wa kikatiba ambao mimi na wenzangu tuliapa
kuutimiza.
Mheshimiwa Spika;
Katika kuongeza uwazi na mawasiliano na wananchi
mwaka 2007 tulianzisha tovuti ya wananchi. Tovuti hiyo
imeshapokea hoja 117,243 na kati ya hizo zilizohusu Serikali
zilikuwa 78,258 na zote zimeshughulikiwa.
Katika kuboresha mfumo wa mawasiliano, Tanzania
imeshahama kutoka mfumo wa analogia na kuingia kwenye
mfumo wa digitali. Hii ni hatua kubwa muhimu kwa
maendeleo ya tasnia ya habari nchini. Jambo ambalo
nasikitika kuwa hatukuweza kulikamilisha ni utungaji wa
Sheria ya Haki ya Upatikanaji wa Habari na Sheria ya
Vyombo vya Habari. Miswada imekamilika na kusomwa
mara ya kwanza hapa Bungeni lakini mchakato wake
haukuweza kufika mwisho. Tunawaachia wenzetu wajao
washughulike nayo katika Bunge la 11.
21
Vita dhidi ya Rushwa
Mheshimiwa Spika;
Vita dhidi ya rushwa ni eneo jingine ambalo tulilivalia
njuga katika Awamu ya Nne. Tumepata mafanikio ya kutia
moyo katika mapambano dhidi ya rushwa ingawaje kazi
bado ni kubwa. Tumefanya mambo matatu. Kwanza,
tumetunga Sheria Na. 11 ya mwaka 2007 ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa ambayo imeongeza nguvu ya
mapambano dhidi ya uovu huu. Idadi ya makosa ya rushwa
iliongezwa kutoka 4 mpaka 24 na wigo wa wakosaji pia,
kwa kuhusisha watu katika sekta binafsi. Mifumo ya
upelelezi na uendeshaji mashitaka nayo imeimarishwa.
Tumeunda chombo kipya TAKUKURU badala ya
TAKURU ambacho kimepewa majukumu ya kuzuia na
kupambana na rushwa badala ya kuzuia peke yake.
TAKUKURU imepewa mamlaka zaidi katika kuongoza
mapambano haya. Taasisi imeendelea kuimarishwa kwa
22
kuipatia zana na vifaa vya kufanyia kazi pamoja na
rasilimali watu na mahitaji mengine. Tumeiwezesha
TAKUKURU kufungua ofisi katika Mikoa na Wilaya zote.
Mheshimiwa Spika;
Maboresho haya yamewezesha idadi ya kesi za tuhuma
za rushwa zinazofikishwa mahakamani kuongezeka kutoka
kesi 50 mwaka 2005 hadi 1,900 mwaka 2014. Jumla ya
shilingi bilioni 87.8 ziliokolewa. Watumishi wa Serikali 97
wameachishwa kazi kwa tuhuma za rushwa na matumizi
mabaya ya ofisi zao baada ya ushahidi wa kijinai
kukosekana. Kwa upande wa kupambana na rushwa
kwenye shughuli za uchaguzi, tumetunga Sheria ya
Kudhibiti Gharama za Uchaguzi Na. 6 ya mwaka 2010 ili
kutoa majibu ya kilio cha siku nyingi dhidi ya watu
wanaotumia fedha kununua kura.
Mapato na Matumizi ya Fedha na Mali za Serikali
Mheshimiwa Spika;
23
Nilieleza katika hotuba yangu ya Kuzindua Bunge la
Tisa tarehe 30 Desemba, 2005 kuwa tutatoa kipaumbele cha
juu kwa ukusanyaji wa mapato ya Serikali na nidhamu ya
matumizi ya Serikali. Leo miaka kumi baadae ninaona
fahari tumepata mafanikio makubwa. Mapato ya Serikali
yameongezeka kutoka shilingi bilioni 177.1 mwaka 2005
kwa mwezi hadi takriban shilingi bilioni 850. Hii
imewezesha bajeti ya Serikali kukua kutoka trilioni 4.13
mwaka 2005/2006 hadi trilioni 22.49 mwaka 2015/2016.
Isitoshe imetuwezesha kupunguza misaada na mikopo ya
washirika wa maendeleo kutoka asilimia 42 ya Bajeti ya
Serikali mwaka 2005 hadi asilimia 15 mwaka 2014/2015 na
tumejipa lengo la kushusha zaidi hadi asilimia 8 mwaka
huu wa fedha wa 2015/2016.
Mheshimiwa Spika;
Mafanikio haya yametokana hasa na kazi kubwa
tuliyoifanya ya kuimarisha Mamlaka ya Mapato ambao
wanastahili pongezi zetu nyingi. Bado naamini tunaweza
24
kufanya vizuri zaidi ya hivi, kama tukiongeza udhibiti kwa
mianya ya kupoteza mapato na kuimarisha zaidi TRA na
mamlaka nyingine za ukusanyaji mapato ya Serikali. Bado
ukusanyaji wa mapato yasiyokuwa ya kodi katika
Halmashauri za Wilaya na Miji na katika Wizara, Idara
zinazojitegemea na Wakala wa Serikali uko chini ya lengo.
Huku kuendelee kufanyiwa kazi.
Mheshimiwa Spika;
Kwa upande wa nidhamu ya matumizi ya fedha na
mali za Serikali tulielekeza nguvu zetu katika kuimarisha
utaratibu wa manunuzi Serikalini na ukaguzi wa hesabu za
Serikali. Kwa upande wa ununuzi wa bidhaa na huduma,
tumeendelea kuimarisha Sheria na Mamlaka ya Ununuzi wa
Umma ili iweze kuhakikisha kuwa kuna usimamizi thabiti
wa sheria hiyo na kanuni zake. Kama mjuavyo sehemu,
kubwa ya fedha za Serikali hutumiwa katika ununuzi wa
bidhaa na huduma, hivyo kuwepo usimamizi mzuri ni
jambo jema. Ukikosekana, wizi na rushwa hutawala.
25
Mheshimiwa Spika;
Kwa upande wa ukaguzi wa hesabu za Serikali,
tumechukua hatua za makusudi za kuimarisha Ofisi ya
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
Tumetunga Sheria mpya inayoipa nguvu na uhuru zaidi
Ofisi hiyo. Aidha, tumewaongezea bajeti, vitendea kazi na
rasilimali watu. Ofisi 8 za Mikoa zimejengwa na 2
zinaendelea kujengwa.
Nafurahi kwamba maagizo yangu kwa viongozi na
watendaji katika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa kuhusu
Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za
Serikali kupewa uzito linazingatiwa. Taarifa hizo sasa
zinasomwa, zinajadiliwa na hatua kuchukuliwa kwa kasoro
zilizoonekana. Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali
imefanya kazi nzuri. Wezi na wabadhirifu wanaobainika
kuchukuliwa hatua za kisheria mara makosa
26
yanapogundulika. Kitaifa taarifa hiyo hujadiliwa Bungeni
kwa muda wa kutosha.
Mheshimiwa Spika;
Niliamua pia kuanzisha Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa
Ndani wa Serikali na kuwaweka Wakaguzi wa Ndani wote
wa Serikali Kuu na Serikali za Mitaa chini ya Mamlaka yake
na kuwajibika kwake. Ofisi hii imesaidia kuhakikisha sheria
na kanuni za matumizi ya fedha na mali ya umma
zinaheshimiwa. Pia, katika ufuatiliaji na utekelezaji wa
mapendekezo ya CAG. Uimarishaji wa ukaguzi wa ndani na
ule wa CAG umesaidia kuboresha hesabu za Serikali kuwa
nzuri zaidi siku hizi. Hati safi zimeongezeka na hati chafu
zinazidi kupungua Serikalini. Kwa mfano katika
Halmashauri za Wilaya na Miji, hati safi zimeongezeka
kutoka 56 mwaka 2006 hadi 150 mwaka 2014. Hati zenye
mashaka ni 13 na hakuna Hati isiyoridhisha. Kazi ya
kuimarisha ukaguzi na nidhamu ya matumizi lazima
iendelezwe.
27
Maadili ya Viongozi wa Umma
Mheshimiwa Spika;
Katika miaka 10 hii tumeimarisha mfumo wa
kusimamia maadili ya viongozi. Tumefanya hivyo kwa
kutambua kuwa maadili mema ni sifa ya msingi ya kiongozi
na huiletea heshima Serikali. Tumeendeleza Kamati ya
Maadili na kuunda Baraza la Maadili kwa mujibu wa Sheria
ya Maadili ya Viongozi wa Umma namba 13 ya 1995.
Tumepanua wigo na kwamba sasa mali za viongozi na
familia zao hutolewa taarifa na kiongozi katika Tamko la
Mali la kila mwaka. Hii inasaidia kuondoa uwezekano wa
kiongozi kuficha mali kwa mgongo wa mwenza wake au
mtoto.
Mheshimiwa Spika;
Kamati ya Maadili sasa si tu inapokea fomu na
kuzihifadhi, bali inafanya ukaguzi wa mali za viongozi na
28
kuzifuatilia. Kikwazo chao ni kupata rasilimali fedha. Hili
litazamwe zaidi. Pale inapoonekana kuna makosa ya
kimaadili wahusika hufikishwa kwenye Baraza la Maadili.
Sote tumeshuhudia kazi nzuri iliyofanywa na Baraza hilo
wakati wa sakata la Escrow. Bado kazi ya kuimarisha
Kamati ya Maadili kwa rasilimali fedha, vitendea kazi,
majengo ya ofisi na rasilimali watu haina budi kuendelezwa.
Muhimili wa Mahakama
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi cha miaka 10 hii tumefanya jitihada
kubwa za kuimarisha mhimili wa Mahakama. Miongoni
mwa mambo mengine, tumefanya mambo muhimu kwa
madhumuni ya kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa
jukumu lake la msingi la utoaji haki.
Kwanza, tumetenganisha shughuli za kutoa haki na za
utawala. Tumeunda Ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama
ya kushughulikia mambo ya fedha na utawala. Hivyo basi,
Wasajili wa Mahakama wanabaki na jukumu la kutoa haki.
29
Mpaka sasa mabadiliko haya yamekuwa ya manufaa
makubwa kwa Mahakama kwani yameboresha utekelezaji
wa majukumu katika Mahakama. Pili, tumeanzisha Mfuko
wa Mahakama ambao unaipa Mahakama uhuru katika
kuendesha shughuli zake. Sambamba na hilo tumeongeza
bajeti ya Mahakama kutoka shilingi bilioni 36.6 mwaka
2006/07 hadi shilingi bilioni 87.6 mwaka 2014/15. Jambo
linalohitaji kuboreshwa ni Hazina kutoa fedha kwa wakati
ili shughuli zifanyike kama ilivyopangwa.
Mheshimiwa Spika;
Jambo la tatu, ni kwamba tumeongeza idadi ya Majaji
wa Rufani, Majaji wa Mahakama Kuu, Mahakimu Wakazi
na Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo. Lengo letu ni
kuongeza nguvukazi ya kusikiliza na kuamua mashauri.
Kwa upande wa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo
wameanza kuteuliwa watu wenye Shahada ya Sheria. Hivi
sasa itawawezesha watu wenye mashauri katika Mahakama
hizo kupata utetezi wa Mawakili. Kati ya mwaka 2005 na
30
2015 tumeongeza Majaji wa Rufani kutoka 8 mwaka 2005
hadi 16, na Majaji wa Mahakama Kuu kutoka 37 hadi 81
katika kipindi hicho. Hali kadhalika, tumeongeza idadi ya
Majaji wanawake. Katika Mahakama ya Rufani wapo 5 na
katika Mahakama Kuu wapo 32 na kufanya jumla yao kuwa
37. Hivi sasa tunao jumla ya Mahakimu Wakazi 1,266 katika
ngazi zote za Mahakama. Kati ya hao 534 sawa na asilimia
35 ni wanawake. Idadi ya Majaji na Mahakimu wanawake
hivi sasa ni kubwa kuliko wakati wowote uliopita.
Mheshimiwa Spika;
Kutokana na mipango mizuri iliyowekwa na Jaji Mkuu
Mohamed Chande Othman Mahakama zimepiga hatua
kubwa katika kupunguza mlundikano wa kesi Mahakamani.
Majaji wamejiwekea malengo kwa kila Jaji asikilize na
kuamua mashauri yasiyopungua 220 kwa mwaka na kila
Hakimu Mkazi mashauri 250 na wale wa Mahakama ya
Mwanzo mashauri 260 kwa mwaka. Kwa sababu hiyo,
kuanzia Julai, 2014 hadi kufikia mwezi Machi mwaka 2015
31
yalifunguliwa mashauri 177,586 na Mahakama ilisikiliza na
kuamua mashauri 179,962. Maana yake ni kuwa
zimesikilizwa zote na nyingine zilizobakia miaka ya nyuma.
Bila shaka kwa kasi hii sasa mrundikano wa kesi utabakia
kuwa historia katika kipindi kifupi kijacho. Nawapongeza
sana Majaji na Mahakimu kwa kazi nzuri waifanyayo.
Kwa upande wa ujenzi wa majengo ya Mahakama
Kuu, wamekamilisha ujenzi wa jengo la Mahakama Kuu za
Divisheni ya Kazi pamoja na majengo ya Mahakama Kuu
Mikoa ya Shinyanga na Kagera. Aidha, majengo mawili ya
Mahakama za Wilaya na 12 ya Mahakama za Mwanzo nayo
yamekamilika. Hivi sasa, ujenzi unaendelea wa majengo ya
Mahakama Kuu 9 za mikoa iliyosalia, Mahakama za Wilaya
9 na za mwanzo 25.
Maboresho ya Mfumo wa Utoaji Haki
Mheshimiwa Spika;
Jambo lingine ambalo tumefanya katika nia ya
kuongeza uwajibikaji, ufanisi, na kupunguza malalamiko ya
32
wananchi na ucheleweshaji wa mashauri ni kutenganisha
kazi ya upelelezi wa makosa ya jinai na uendeshaji wa
mashtaka hayo Mahakamani. Polisi waliokuwa wanafanya
yote sasa watashughulikia upelelezi na ofisi ya Mkurugenzi
wa Mashtaka ndiyo inayoendesha mashauri. Tayari Ofisi za
Mkurugenzi wa Mashtaka zimekwishafunguliwa katika kila
Mkoa na sasa tunaenda wilayani. Aidha, tumeboresha Ofisi
ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa rasilimali watu,
vitendea kazi na fedha ili kuongeza ufanisi katika utendaji
wa ofisi hiyo muhimu sana. Kuna haja ya kuendelea
kuongezea rasilimali fedha na vitendea kazi ili ufanisi
uongezeke zaidi.
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki, tumeimarisha Tume ya Haki za
Binadamu na Utawala Bora kwa kuiwezesha kwa nyenzo,
rasilimali fedha na watu. Tume sasa inafanya kazi katika
eneo lote la Jamhuri ya Muungano. Aidha, kutokana na
33
utumiaji wa mfumo wa elektroniki malalamiko ya wananchi
mengi zaidi yanafikishwa kwenye Tume na mengi
yanapatiwa ufumbuzi. Kwa mfano, idadi ya malalamiko
yaliyowasilishwa Tume yameongezeka kutoka 9,455
mwaka 2006 hadi 25,921 mwaka 2014 na uwezo wa Tume
kushughulikia malalamiko kwa mwaka umeongezeka
kutoka malalamiko 3,021 mwaka 2005 hadi malalamiko
18,501 mwaka 2014.
Utendaji Serikalini
Maeneo ya Utawala
Mheshimiwa Spika;
Kwa nia ya kusogeza huduma, mwaka 2010 tulianzisha
mikoa mipya 4 ya Geita, Simiyu, Njombe na Katavi na
wilaya mpya 19. Pia, tulianzisha Halmashauri 45, kata 1,432,
vijiji 1,949, Mitaa 1,379 na vitongoji 8,777. Nimeamua
kuanzisha mkoa mpya wa Songwe kutoka mkoa wa Mbeya
na Wilaya sita kama ifuatavyo: Tanganyika mkoani Katavi,
Kigamboni na Ubungo mkoani Dar es Salaam, Songwe
34
mkoani Mbeya, Kibiti mkoani Pwani na Malinyi mkoani
Morogoro. Najua tulikuwa na maombi mengi lakini kwa
sasa tufanye haya.
Maslahi ya Wafanyakazi
Mheshimiwa Spika;
Serikali ya Awamu ya Nne imelipa umuhimu wa juu
suala la kuboresha maslahi ya watumishi wa Serikali. Karibu
kila mwaka tumekuwa tunaongeza kima cha chini cha
mshahara. Kwa sababu hiyo, kima cha chini cha mshahara
kimeongezeka kutoka shilingi 65,000 mwaka 2005 hadi
shilingi 265,000 mwaka wa jana. Mwaka huu tumefikia
shilingi 300,000. Najua bado hakikidhi mahitaji lakini
ukilinganisha na tulikokuwa kipindi hiki tumeongeza sana
mishahara ya wafanyakazi. Vile vile, tumeendelea
kupunguza kodi ya mapato kwa mfululizo kutoka asilimia
18 mwaka 2005 hadi asilimia 11 mwaka huu. Dhamira yetu
ni kutaka kutoa nafuu zaidi kwa wafanyakazi. Vile vile,
tumewapandisha vyeo watumishi 233,876 na kulipa
35
malimbikizo ya watumishi 422,348 ya kiasi cha shilingi
bilioni 384.8.
Mheshimiwa Spika;
Tumetekeleza sera ya ugatuaji wa madaraka kwa
wilaya jambo ambalo limelazimu kuongeza rasilimali fedha
na watu kwa Halmashauri za Wilaya na Miji. Kwa ajili hiyo
ruzuku kwa Halmashauri zetu imeongezeka kutoka shilingi
bilioni 780 mwaka 2005/2006 hadi shillingi trilioni 4.69
mwaka 2015/2016. Aidha, tumeimarisha utumishi katika
Halmashauri kwa kuajiri watumishi wengi wa kada
mbalimbali.
Usawa wa kijinsia
Mheshimiwa Spika;
Mwaka 2005 niliahidi wakati wa kampeni na wakati wa
kuzindua Bunge la Tisa, kuwa tutaongeza ushiriki wa
wanawake katika shughuli na nyanja mbalimbali za maisha
ya watu wa nchi yetu ikiwemo nafasi za maamuzi. Ninyi na
mimi ni mashahidi kwamba tumetimiza ahadi hiyo. Idadi
36
ya Wabunge wanawake imeongezeka kutoka 62 mwaka
2005 hadi 127. Hivi sasa hamsini kwa hamsini ni rasmi
katika Katiba Inayopendekezwa. Kwa mara ya kwanza
katika historia ya nchi yetu na Bunge letu tumepata Spika
mwanamke Mheshimiwa Anne Semamba Makinda.
Wanawake wameongezeka katika ngazi zote kuu za
uamuzi. Kwa mfano, tunao Mawaziri wanawake 10, Naibu
Mawaziri wanawake 5, Majaji wanawake 37 na Wakuu wa
Wilaya wanawake wako 53. Kwa upande wa Makatibu
Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa,
Wakurugenzi Watendaji n.k. pia wameongezeka. Katika
elimu nako tuna usawa wa kijinsia kwa upande wa idadi ya
wanafunzi wa kike na wa kiume katika shule za msingi na
sekondari. Katika vyuo vya elimu ya juu, idadi ya
wanafunzi wa kike imeongezeka kwa kasi kutoka 10,039
mwaka 2005 hadi 78,800 mwaka 2014.
37
Hali ya Uchumi
Mheshimiwa Spika;
Wakati ninaingia madarakani mwaka 2005 niliwaahidi
Watanzania wenzangu kuwa tutafanya kila tuwezalo
kujenga uchumi ulio imara na shirikishi. Hususan, nilisema
nitaendeleza sera za mageuzi ya kiuchumi na kuweka
misingi madhubuti ya kukuza uchumi, kuongeza ajira,
kuongeza Pato la Taifa na kupunguza umaskini. Katika
miaka kumi iliyopita tumeendelea kusimamia kwa kiwango
kizuri sera za uchumi jumla na sera za uchumi katika ngazi
ya chini zinazogusa wananchi wa kawaida.
Jitihada zetu hizo zimezaa matunda ya kutia moyo.
Katika kipindi hiki, Pato la Taifa lilikua kwa wastani wa
takriban asilimia 7. Nchi yetu ni miongoni mwa mataifa 10
ya Afrika na 20 duniani ambayo uchumi wake unakua kwa
kasi kubwa. Pato ghafi la Taifa limeongezeka zaidi ya mara
tatu kutoka shilingi trilioni 14.1 mwaka 2005 hadi kufikia
trilioni 79.4 mwaka 2014. Hivyo basi, pato la wastani la
38
Mtanzania nalo limeongezeka kutoka shilingi 441,030
mwaka 2005 hadi shilingi 1,724,416 mwaka 2014.
Mheshimiwa Spika;
Mauzo yetu ya nje yameongezeka kutoka Dola za
Marekani bilioni 1.67 mwaka 2005 hadi Dola za Marekani
bilioni 8.76 mwaka 2014 na kutunisha akiba yetu ya fedha
za kigeni na kutuwezesha kuagiza bidhaa na mahitaji ya
nchi kutoka nje kwa kipindi cha miezi 4.1 kama
tulivyopanga. Mfumuko wa bei ni asilimia 6.1.
Mheshimiwa Spika;
Kama mjuavyo, mwaka 2000 nchi yetu ilijiwekea Dira
ya Taifa ya Maendeleo ya hadi mwaka 2025. Mwaka 2010
tulitengeneza Mpango wa Muda Mrefu (Long Term
Perspective Plan) wa (2010 2025) wa kuongoza utekelezaji
wa Dira kwa miaka 15 iliyobaki. Tuligawa utekelezaji wake
katika Mipango mitatu ya Maendeleo ya Miaka Mitano kila
mmoja. Tuko katika hatua za mwisho za utekelezaji wa
39
Mpango wa Kwanza, (2011/12 2015/16) na kuandaa
mpango wa pili (2016/17 2021/22).
Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa
Mheshimiwa Spika;
Kwa madhumuni ya kuboresha utendaji wa Serikali
nilianzisha Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Huu ni mfumo mpya wa kupanga, kufuatilia na kusimamia
utekelezaji wa malengo na shughuli za Serikali kwa nia ya
kuhakikisha kuwa kilichokusudiwa kinafanyika, tena kwa
wakati. Tuliamua kuanza na sekta sita za Elimu, Nishati,
Kilimo, Uchukuzi, Maji na Mapato ya Serikali. Baadae
sekta ya afya na uboreshaji mazingira ya uwekezaji
ziliongezwa.
Katika kipindi hiki kifupi Mpango umethibitisha kuwa
wenye manufaa. Mambo katika sekta zilizojumuishwa
katika BRN yameanza kwenda vizuri. Changamoto yetu
kubwa imekuwa ni upatikanaji wa fedha zinazohitajika kwa
40
wakati kutoka Hazina. Kama changamoto hiyo
isingekuwepo mambo yangekuwa mazuri zaidi.
Uboreshaji wa Mazingira ya Biashara na Uwekezaji
Mheshimiwa Spika;
Kwa kutambua umuhimu wa uwekezaji katika kukuza
uchumi, kuzalisha ajira, kuongeza mapato na kupunguza
umaskini, Serikali yetu imekuwa inachukua hatua thabiti za
kutengeneza mazingira mazuri ya kuwavutia wawekezaji
wa ndani na nje kuchagua Tanzania kuwa nchi inayofaa
kuwekeza.
Mwaka 2010 tumetengeneza Sera na kutunga Sheria ya
Ubia baina ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (Public
Private PartnershipPPP). Lengo letu ni kuweka mazingira
mazuri kwa sekta binafsi kuvutika kushirikiana na Serikali
katika shughuli za kiuchumi na maendeleo. Faida kubwa ya
utaratibu huu ni kuipunguzia Serikali mzigo wa kuwekeza
katika baadhi ya shughuli ambazo sekta binafsi inaweza
kubeba sehemu ya gharama. Hii siyo tu inaongeza kasi ya
41
maendeleo, bali kuiwezesha Serikali kuokoa fedha ambazo
inaweza kuzitumia kwa shughuli nyingine.
Juhudi zetu za kuboresha mazingira ya uwekezaji
zinaendelea kuzaa matunda mema. Kati ya 2005 na 2014,
Kituo chetu cha Uwekezaji (TIC) kimesajili miradi 7,159
yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 154.274. Kati ya
miradi hiyo asilimia 49.38 ni ya wawekezaji wa ndani,
asilimia 23.41 ni wawekezaji wa kutoka nje na asilimia 27.18
ni miradi ya ubia baina ya Watanzania na wawekezaji wa
kigeni. Ajira 16,000 zilipatikana. Ukuaji huu wa uwekezaji
umeongeza mapato ya Serikali.
Kwa mujibu wa taarifa ya uwekezaji iliyotolewa na
Shirika la Umoja wa Mataifa la Viwanda na Biashara
Duniani (UNCTAD) ya mwaka 2015, Tanzania inaongoza
Afrika Mashariki kwa kuvutia uwekezaji. Ilipata Dola za
Marekani bilioni 2.142 sawa na asilimia 31.5 ya uwekezaji
wote katika Jumuiya yetu.
42
Sekta za Uzalishaji
Sekta ya Kilimo
Mheshimiwa Spika;
Kuendeleza kilimo ilikuwa ni moja ya mambo
tuliyoyapa kipaumbele cha juu. Shabaha yetu kuu ni kutaka
kuongeza tija ili uzalishaji uongezeke, wakulima wapate
mavuno mengi, masoko ya uhakika yawepo na bei iwe nzuri
ili mapato yao yaongezeke na umasikini uwapungukie. Vile
vile wao na taifa lijitosheleze kwa chakula.
Kwa ajili hiyo mwaka 2006 tuliasisi Programu ya miaka
7 ya Maendeleo ya Sekta ya Kilimo (Agricultural Sector
Development ProgrammeASDP). Katika Programu hiyo,
matatizo yanayofanya tija na uzalishaji katika kilimo kuwa
mdogo yalitambuliwa na kutengenezewa mpango wa
kuyatatua. Serikali pia ilianzisha mikakati, programu na
mipango mingine ya kuongeza msukumo katika kuleta
mageuzi ya kilimo. Miongoni mwa hiyo ni mkakati wa
Kilimo Kwanza, Mpango wa Kuendeleza Kilimo katika
43
Ukanda wa Kusini mwa Tanzania (SAGCOT), Mpango wa
Uwekezaji katika Sekta ya Kilimo (TAFSIP), Sera ya
Umwagiliaji tuliyoitunga mwaka 2010 na Programu ya
Mageuzi na Modenaizesheni ya Ushirika.
Mheshimiwa Spika;
Pamoja na hayo, tumeongeza pia bajeti ya sekta ya
kilimo kutoka shilingi bilioni 233.3 mwaka 2005/06 hadi
shilingi bilioni 1,084.7 mwaka 2014/15. Kuongezwa kwa
bajeti kumewezesha fedha za ruzuku ya mbolea na
pembejeo kuongezeka kutoka shilingi bilioni 7.5 mwaka
2005/06 hadi shilingi bilioni 299.3 mwaka 2013/14. Matrekta
makubwa na madogo yameongezeka kutoka 7,491 mwaka
2005 hadi 16,412 mwaka 2014. Kwa sababu hiyo matumizi
ya jembe la mkono yamepungua kutoka asilimia 70 hadi
asilimia 62. Tumeongeza maafisa ugani kutoka 3,379 mwaka
2005 hadi 7,974 mwaka 2014.
Vituo vya utafiti wa kilimo tumeviongezea rasilimali
fedha, watu na vitendea kazi. Aidha, tumeanza safari ya
44
kufufua mashamba ya mbegu ya Serikali na kuhusisha sekta
binafsi, Jeshi la Magereza na Jeshi la Kujenga Taifa katika
kuzalisha mbegu. Aidha, tumeimarisha Wakala wa Mbegu
(Agricultural Seed Agency ASA) na kuongeza uzalishaji
wa mbegu bora kutoka tani 10,477.17 mwaka 2005 hadi tani
32,340 mwaka 2014.
Mheshimiwa Spika;
Juhudi za Serikali kuendeleza kilimo zimezaa matunda
mazuri. Tija katika uzalishaji wa mazao ya biashara na
chakula imeongezeka. Kwa upande wa mazao ya chakula
uzalishaji umeongezeka kutoka tani milioni 9.66 mwaka
2005 hadi tani milioni 16.01 mwaka 2014. Ongezeko hili
limeliwezesha taifa letu kujitosheleza kwa chakula kwa
asilimia 125 mwaka 2014 ikilinganishwa na asilimia 95
mwaka 2005. Uzalishaji wa mazao ya asili ya biashara
umeongezeka toka tani 427,738 mwaka 2005 hadi tani
569,054 mwaka 2014 na uzalishaji wa mbegu za mafuta
umeongezeka karibu ya mara 4 toka tani 1,389.9 mwaka
45
2005 hadi tani 5,545.6 mwaka 2014. Aidha, uzalishaji wa
matunda nao umeongezeka toka tani milioni 1.2 mwaka
2005 hadi tani milioni 4.4 mwaka 2014 na maua toka tani
5,862 hadi tani 10,790.
Mheshimiwa Spika;
Upatikanaji wa masoko ya uhakika na bei nzuri kwa
mazao ya wakulima bado ni changamoto. Pia kuna tatizo la
upungufu wa maghala ya kuhifadhi mazao. Jitihada
zinaendelea kupata mkopo au wabia wa kujenga maghala
ya kisasa nchi nzima. Programu ya Mageuzi na
Modenaizesheni ya Ushiriki ilianzishwa ili kutatua tatizo la
masoko. Aidha, tumeanza maandalizi ya kuanzisha soko la
bidhaa (Commodity Market Exchange) kwa nia hiyo hiyo.
Naamini misingi mizuri tuliyoijenga pamoja na kuenea kwa
SACCOS na kuanza kwa Benki ya Kilimo ikiendelezwa
itatoa mchango mkubwa katika kuongeza kasi ya
mapinduzi ya kilimo.
46
Mifugo
Mheshimiwa Spika;
Kwa upande wa mifugo, dhamira yetu ilikuwa kuanza
safari ya kuleta mageuzi katika sekta hii. Safari hiyo
tumeianza kupitia Programu ya Kuendeleza Sekta ya
Mifugo. Changamoto zinazochangia maendeleo duni ya
sekta hii zimeainishwa na kutengenezewa mkakati wa
utekelezaji. Katika kipindi hiki malambo 1,008, majosho
2,364 na maabara 104 za mifugo zimejengwa. Visima virefu
101 vimechimbwa, malambo 370 na majosho 499
yamekarabatiwa katika kipindi hiki cha miaka 10.
Ukarabati na ujenzi wa majosho umeongeza idadi
kutoka 2,177 mwaka 2006 hadi 3,637 mwaka 2015.
Tumeongeza Maofisa Ugani kutoka 2,270 mwaka 2005 hadi
6,041 mwaka 2014. Kuhusu uhamilishaji, tumeongeza vituo
kutoka kituo 1 mwaka 2005 hadi vituo 8 mwaka 2015 na
kuwezesha ngombe 955,360 kuhamilishwa katika miaka 10
hii.
47
Mheshimiwa Spika;
Mazingira mazuri ya uwekezaji kwa sekta binafsi
tuliyoyajenga yamewezesha viwanda vya kusindika nyama,
maziwa na vyakula vya mifugo kuongezeka. Viwanda vya
kusindika maziwa vimeongezeka kutoka 22 mwaka 2005
hadi 74 mwaka 2015. Viwanda vya kuzalisha vyakula vya
mifugo vimeongezeka kutoka viwanda 6 mwaka 2005 hadi
80 mwaka 2015 vikiwa na uwezo wa kusindika tani milioni
1.4 za vyakula hivyo kwa mwaka. Aidha viwanda na
machinjio ya kisasa 9 vimejengwa katika kipindi hiki.
Usindikaji wa ngozi pia umeongezeka kutoka vipande
790,000 mwaka 2005 hadi vipande milioni 3.78 mwaka 2014.
Hivi sasa kwa mfano, uzalishaji wa malisho ya mifugo (hei)
umefikia marobota 957,860 ikilinganishwa na marobota
178,100 mwaka 2005.
Safari yetu ya kuanza kuondoka kwenye uchungaji
kwenda kwenye ufugaji imeanza. Vijiji vingi vimeandaa
mipango ya matumizi bora ya ardhi na hivyo vimetenga
48
maeneo ya kilimo na ya ufugaji. Tuendelee kuhimiza vijiji
vyetu kutekeleza mipango hiyo ili wafugaji wapate maeneo
ya malisho mbali na mazao ya wakulima. Pia, tuhimize
uhamilishaji kama mlango wa kuingilia kwenye kuboresha
kosafu za mifugo yetu.
Uvuvi
Mheshimiwa Spika;
Wakati nazindua Bunge la Tisa tarehe 30 Desemba 2005
nilisema kuwa Serikali ya Awamu ya Nne itatoa kipaumbele
kwenye kuendeleza sekta ya uvuvi. Katika kutekeleza hayo
tumefanya yafuatayo. Kwanza, nimeunda Wizara mpya ya
Mifugo na Uvuvi. Pili, tulifuta kodi ya zana za uvuvi ili
kuwawezesha wavuvi kupata zana bora na za kisasa kwa
bei nafuu zaidi. Tatu, tumeimarisha vyuo vya uvuvi na hivi
sasa vina uwezo wa kudahili wanafunzi 1,215
ikilinganishwa na wanafunzi 127 mwaka 2005. Hii
imetuwezesha kuongeza wagani wa uvuvi kutoka 103
mwaka 2005 hadi 540 mwaka 2014. Nne, tumeongeza sana
49
juhudi za kupambana na uvuvi haramu ili kutunza
mazingira, mazalia ya samaki na kuzuia kuvuliwa au
kuuawa kwa samaki wadogo.
Tumeimarisha maabara ya Taifa ya Samaki pale
Nyegezi kwa vifaa vya kisasa na wataalamu ili iende na
wakati. Tano, tumeongeza msukumo wa kuhimiza ufugaji
wa samaki na kuwezesha mashamba ya samaki kuongezeka
kutoka 13, 011 mwaka 2005 hadi 20, 325 mwaka 2014.
Uvuvi haramu unapungua. Mapato ya sekta ya uvuvi
yameongezeka kutoka shilingi bilioni 351.6 mwaka 2005
hadi shilingi trilioni 1.8 mwaka 2013. Bado tuna kazi kubwa
ya kufanya katika sekta hii ili kuongeza tija na mapato ya
wavuvi na taifa.
Utalii
Mheshimiwa Spika;
Kwa upande wa utalii, tumeendelea na jitihada za
kuiendeleza sekta hii muhimu. Tumeongeza kutangaza
vivutio vya utalii vya nchi yetu katika masoko makubwa
50
duniani. Sekta ya utalii imekua kwa wastani wa asilimia 7.1
na imechangia asilimia 25 ya mapato ya fedha za kigeni.
Idadi ya watalii imeongezeka kutoka watalii 612, 754 mwaka
2005 hadi watalii 1,140,156 mwaka 2014. Idadi ya vitanda
katika mahoteli imeongezeka kutoka 15,828 hadi 21,929.
Mapato pia yameongezeka kutoka Dola za Marekani
milioni 823.05 mwaka 2005 hadi Dola za Marekani bilioni 2
mwaka 2014. Ajira za moja kwa moja zimeongezeka kutoka
32,673 hadi 686,130 na zisizokuwa za moja kwa moja kutoka
165,883 hadi 1,318,109. Haya ni mafanikio makubwa na ya
kujivunia.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki tumekabiliana na tukio kubwa la
ujangili wa wanyamapori hasa wa ndovu kutokana na
kushamiri kwa biashara ya meno ya ndovu na bei kuwa
kubwa katika nchi za Mashariki ya Mbali. Vuguvugu la
ujangili lilifikia kiwango cha kutishia kumaliza ndovu
nchini na dunia nzima. Tukaamua kuchukua hatua za
51
kuidhibiti hali hiyo. Tumefanya operesheni tatu kukabiliana
na tishio hili. Ya kwanza, iliendeshwa na Idara ya
Wanyamapori na Misitu wakishirikiana na TANAPA na
Ngorongoro Conservation Area. Hii hasa ilihusu
kupambana na ujangili katika hifadhi na mapori ya
Kaskazini mwa Tanzania. Mafanikio makubwa yalipatikana.
Mheshimiwa Spika;
Operesheni ya pili ni ile iliyohusisha Jeshi la Polisi
katika hifadhi na sehemu nyingine za Tanzania. Operesheni
Kipepeo kama ilivyoitwa nayo ilipata mafanikio. Na ya tatu,
Operesheni Tokomeza iliyohusisha vyombo vyote vya ulinzi
na usalama. Pamoja na changamoto zake operesheni hizi
zimesaidia sana kupunguza kasi ya ujangili nchini. Matokeo
yake katika sensa ya ndovu iliyofanyika mara ya mwisho,
ukiacha Ruaha, hali katika hifadhi na mapori mengine ina
muelekeo mzuri.
Kuundwa kwa Mamlaka ya Wanyamapori (TAWA)
yenye mamlaka makubwa zaidi ya kusimamia sekta ya
52
wanyamapori nako kutaimarisha uhifadhi na mapambano
ya ujangili. Kwa mipango na program zilizopo Wizarani,
naamini mambo yatakuwa mazuri zaidi muda si mrefu.
Viwanda
Mheshimiwa Spika;
Katika miaka kumi hii, sekta ya viwanda imeendelea
kukua kwa kasi nzuri ya kutia moyo. Viwanda vikubwa,
vya kati na vidogo vimeongezeka kutoka 11, 544 mwaka
2005 hadi viwanda 51,224 mwaka 2015. Kati ya mwaka 2005
na 2014 na miradi 751 imepewa leseni za kudumu na BRELA
ya kuanzisha viwanda. Mchango wa sekta ya viwanda
katika Pato la Taifa umefikia asilimia 7.3 mwaka 2014
kutoka asilimia 6.8 mwaka 2005. Mchango wa viwanda
kwenye mauzo ya nje umeongezeka kutoka asilimia 9.3
mwaka 2005 hadi asilimia 23.3 mwaka 2014.
Tunategemea ukuaji mkubwa wa viwanda katika
Mpango wa Pili wa maendeleo wa miaka 5 kutokana na
misingi imara tuliyoijenga katika Mpango wa Kwanza.
53
Ujenzi wa kiwanda cha chuma kule Liganga na makaa ya
mawe cha Mchuchuma, unatarajiwa kuanza mwaka huu na
kiwanda cha kuchakata gesi pale Lindi unatarajiwa kuanza
baada ya taratibu za kuwapatia ardhi zitakapokamilika.
Hivi ni viwanda vya msingi na mama ambavyo vitachochea
kasi ya ukuaji wa viwanda nchini na uchumi kwa jumla.
Madini
Mheshimiwa Spika;
Sekta ya Madini ndiyo ya pili baada ya utalii kwa
kuingiza fedha nyingi za kigeni. Kama nilivyoahidi, tulipitia
upya sera, sheria na mikataba ya madini iliyokuwepo na
kutengeneza sera na sheria mpya. Halikadhalika,
tulianzisha mazungumzo na baadhi ya makampuni ambayo
hatimaye yalizaa marekebisho ya mikataba yao na hivyo
kuboresha maslahi ya taifa.
Kufuatia marekebisho hayo, makampuni husika ya
madini yanalipa kodi ya mapato. Bila ya hivyo huenda
mpaka leo yangekuwa hayajaanza kulipa kodi. Kutumika
54
kwa Sheria mpya ya Madini, viwango vipya vya mrahaba na
kupunguzwa kwa misamaha ya kodi vimeongeza mapato ya
Serikali. Aidha, tuliunda Wakala wa Ukaguzi wa Madini
Tanzania (TMAA) ambao umewezesha kukagua mahesabu
ya migodi kuhusu uwekezaji na mauzo ya madini na
kuwawezesha TRA kutoza kodi stahiki kutoka kwa
makampuni hayo.
Mheshimiwa Spika;
Mabadiliko haya pamoja na kuongezeka kwa
uwekezaji katika sekta hii yamewezesha mchango wa sekta
ya madini katika Pato la Taifa kuongezeka kutoka asilimia
2.9 mwaka 2005 hadi kufikia asilimia 3.5 mwaka 2014.
Thamani ya mauzo ya madini nje ya nchi pia imeongezeka
kutoka Dola za Marekani milioni 655.5 mwaka 2005 hadi
kufikia Dola za Marekani bilioni 1.794 mwezi Desemba
2014. Mambo yangekuwa mazuri zaidi kama bei ya dhahabu
isingeshuka katika kipindi hiki.
55
Mheshimiwa Spika;
Serikali ilifanya uamuzi wa kulifufua na kuliwezesha
Shirika letu la Madini (STAMICO) kuanza tena kazi ya
utafutaji na uchimbaji wa madini kupitia kampuni zake
tanzu. STAMICO kwa kupitia kampuni yake ya
STAMIGOLD imeanza kuzalisha dhahabu na kuuza nje.
Vilevile, tumejiunga na Mpango wa Uwazi wa Uvunaji wa
Maliasili (EITI) ambao umesaidia sana katika kuongeza
uwazi katika biashara ya madini na kusaidia katika
ukusanyaji wa mapato kutoka kwenye makampuni ya
madini.
Katika kipindi hiki, migodi mitatu mipya ilianzishwa
nayo ni Migodi ya dhahabu wa Buzwagi (Shinyanga) na
New Luika (Mbeya) na mgodi wa makaa ya mawe wa
Ngaka (Ruvuma). Aidha, miradi mikubwa mingine 8
imeendelezwa na kufikia hatua ya kuanzisha mgodi
ukiwemo Mradi wa Urani wa Mkuju (Ruvuma), Mradi wa
Chuma Liganga na Mradi wa Makaa ya Mawe wa
56
Mchuchuma (Njombe). Pia, ajira rasmi kwenye migodi
mikubwa nchini imeongezeka kutoka waajiriwa 3,517
mwaka 2005 hadi waajiriwa 15,000 mwaka 2014. Hali
kadhalika, makampuni ya madini yameongeza unununzi
wa bidhaa na huduma hapa nchini (local procurement)
kutoka Dola za Marekani milioni 230.41 mwaka 2005 hadi
Dola za Marekani milioni 536.56 mwaka 2014.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki pia, tumetenga maeneo 8 kwa ajili
ya wachimbaji wadogowadogo. Maeneo haya yamewezesha
wachimbaji wadogo kuchimba madini bila bughudha.
Aidha, Wizara imenunua mitambo miwili kwa ajili ya
uchorongaji wa miamba kusaidia utafiti wa madini kwa ajili
ya wachimbaji wadogo. Tumeanzisha mfuko wa
kuwakopesha wachimbaji wadogo pale Wizarani ili kutoa
fursa kwa wachimbaji wadogo kupata mikopo ya
kuendeleza shughuli zao.
57
Nishati
Mheshimiwa Spika;
Wakati naanza kazi ya uongozi wa nchi yetu, Tanzania
ilikuwa inakabiliwa na ukame mkubwa uliosababisha
upungufu mkubwa wa chakula. Pia kulikuwa na upungufu
mkubwa wa umeme kwa sababu ya mabwawa ya kuzalisha
umeme kukosa maji ya kutosha. Serikali ililazimika kulisha
watu zaidi ya milioni 3,776,000 na kukodisha mitambo ya
kuzalisha umeme. Kwa siku za usoni tuliamua kuchukua
hatua thabiti ya kuongeza uzalishaji wa umeme kwa
kutumia gesi asilia na vyanzo vingine kama vile makaa ya
mawe, mionzi ya jua na upepo.
Ujenzi umekamilika wa bomba la kusafirisha gesi
kutoka Mtwara na Songo Songo litakaloongeza kiasi cha gesi
kuja Dar es Salaam na kuwezesha uzalishaji wa megawati
3000 za umeme. Wakati huo huo kazi ya kujenga vituo vya
kufua umeme inaendelea pale Kinyerezi, Dar es Salaam.
58
Umeme huo utakidhi mahitaji ya umeme sasa na miaka
kadhaa ijayo.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki tuliunda Wakala wa Umeme
Vijijini (REA) ambao wamefanya kazi kubwa na nzuri ya
kusambaza umeme kwa vijiji 5,336 kati ya vijiji 12,423
nchini. Kazi kubwa iliyofanyika vijijini inapochanganywa
na ile ya mijini imeongeza idadi ya Watanzania wanaopata
umeme kutoka asilimia 10 hadi asilimia 40 mwaka 2015.
Uamuzi uliofanywa katika Bajeti ya mwaka huu wa
kukusanya fedha kwa ajili ya umeme vijijini kupitia mafuta
ya petroli, utasaidia sana kuongeza kasi ya kusambaza
umeme vijijini.
Gesi Asilia
Mheshimiwa Spika;
Tumepata mafanikio katika utafutaji wa mafuta na gesi
asilia. Kuanzia mwaka 2010 nchi yetu imepata bahati ya
ugunduzi wa kiasi kikubwa cha gesi bahari kuu. Mpaka sasa
59
zimegundulika futi za ujazo trilioni 47.08. Ukijumlisha na
futi za ujazo trilioni 8 zilizogunduliwa takriban miaka 40
iliyopita kule Songo Songo na Msimbati jumla ya rasilimali
ya gesi asilia nchini ni futi za ujazo trilioni 55.08. Kazi ya
utafutaji inaendelea na wataalamu wanasema kuwa
Tanzania inaweza kuwa na akiba ya futi za ujazo trilioni
200. Kiasi cha gesi kilichogunduliwa mpaka sasa ni
kikubwa na kufanya Tanzania kuwa mahala papya pa
kuipatia dunia nishati hii.
Gesi asilia tuliyonayo ikisimamiwa na kutumiwa vizuri
itaiwezesha nchi yetu na watu wake kupata maendeleo
makubwa na kuondokana na umaskini. Ni fursa ya aina
yake ya kuipatia Serikali mapato makubwa na kuiwezesha
kutimiza kwa uhakika majukumu yake na mipango yake.
Lakini, ili hayo yaweze kufanyika hapana budi pawepo
usimamizi mzuri wa hatua zote muhimu za mnyororo wa
thamani: yaani utafutaji, uchimbaji, usafirishaji, uuzaji wa
gesi asilia na matumizi yake nchini kama nishati na mali
60
ghafi ya viwanda upande mmoja. Upande mwingine
inategemea sana matumizi mazuri ya mapato yatokanayo na
rasilimali hiyo.
Mheshimiwa Spika;
Ni kutokana na kutaka kuhakikisha kwamba mambo
yanakuwa hivyo ndiyo maana tumetunga Sera ya Gesi
Asilia na kuwasilisha katika Bunge hili ile Miswada miwili
yaani wa Sheria ya Petroli na ule wa Matumizi ya Mapato ya
Mafuta na Gesi. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge
kwa kuipitisha Miswada hii nami nitaitia saini mara
nitakapoletewa.
Usafirishaji na Uchukuzi
Barabara
Mheshimiwa Spika;
Serikali ya Awamu ya Nne, imetoa kipaumbele cha juu
kwa uendelezaji wa miundombinu ya usafirishaji na
uchukuzi nchini. Hii ni pamoja na barabara, reli, bandari,
usafiri wa majini na usafiri wa angani. Tumeendeleza kazi
61
ya kuongeza mtandao wa barabara za lami nchini kwa
mafanikio makubwa. Karibu barabara kuu zote nchini na
zile zinazounganisha mikoa zimekamilika kujengwa au kazi
ya ujenzi inaendelea. Kwa sababu hiyo hivi leo kutokea po
pote nchini kwenda Dar es salaam unafika siku hiyo hiyo,
tofauti na ilivyokuwa zamani watu walichukua zaidi ya siku
moja. Adha ya kupita Kenya na Uganda kwa watu wa
Mikoa ya Ziwa tumeimaliza.
Katika mkakati wetu wa kupanua mtandao wa
barabara za lami nchini, tulitambua barabara za urefu wa
kilomita 11,474 za kujengwa kwa kiwango cha lami. Baadae
tuliongeza barabara nyingine na kufikisha kilomita 17,742
katika mpango huo. Utekelezaji wake upo katika hatua
mbalimbali. Tayari ujenzi wa kilomita 5,568 kwa upande
wa barabara kuu na kilomita 535 kwa barabara za mijini
umekamilika. Ujenzi wa kilomita 3,873 unaendelea.
Upembuzi yakinifu na usanifu umekamilika kwa barabara
za urefu wa kilometa 4,965 kinachosubiriwa ni kupatikana
62
fedha ujenzi uanze. Baadhi ya barabara hizo zimo katika
bajeti ya mwaka huu wa fedha. Barabara za urefu wa
kilometa 3,336 zinafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu
wa kina.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki pia, madaraja madogo 7,200 na
makubwa 12 yamejengwa na mengine 16 yapo katika hatua
mbalimbali za ujenzi. Miongoni mwa madaraja makubwa
yaliyokamilika ni daraja la Mto Malagalasi na yanayojengwa
ni daraja la Kigamboni na lile la Mto Kilombero. Madaraja
haya yalikuwa miongoni mwa matano yaliyopangwa
kujengwa katika Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa
Miaka Mitano mara baada ya uhuru. Madaraja mawili yaani
la Kirumi lilijengwa mwaka 1985 na la Rufiji mwaka 2003.
Kwa upande wa vivuko, tumeongeza vipya 15 na kufikisha
idadi ya 28 kote nchini mwaka 2014.
63
Mheshimiwa Spika;
Tumeongeza sana fedha katika mfuko wa barabara
kutoka shilingi bilioni 73.08 mwaka 2005/06 hadi shilingi
bilioni 866.63 mwaka 2015/16. Hii itasaidia katika
matengenezo ya barabara za lami tulizojenga na kujenga
nyingine mijini. Hali kadhalika itatumika kuimarisha
barabara za udongo na changarawe wilayani na vijijini
ziweze kupitika wakati wote. Katika kipindi hiki barabara
za changarawe zimeongezeka kutoka kilometa 9,424 hadi
kilometa 22,089.
Mheshimiwa Spika;
Katika miaka kumi hii idadi ya vyombo vya moto yaani
magari, bajaji na pikipiki imeongezeka kutoka 1,696,088
mwaka 2005 hadi 3,313,254 hivi sasa. Ongezeko hili
linalotokana na hali ya kiuchumi ya watu wengi kuwa nzuri
limezua tatizo la msongamano wa magari katika miji mingi
nchini. Katika jiji la Dar es Salaam ambako tatizo ni kubwa
zaidi na Serikali imekuwa inachukua hatua mbalimbali
64
kupunguza ukali wake. Tunapanua ukubwa wa baadhi ya
barabara, kujenga barabara za mzunguko (ring roads) na
sasa tunaanza ujenzi wa barabara za juu ya nyingine
(flyovers). Tulianzisha matumizi ya treni katika reli za
TAZARA na TRC kusafirisha abiria. Hivi sasa reli hizo
zinasafirisha abiria milioni 2,804,269 kwa mwaka ambao
wangehitaji daladala 253 kwa siku. Mpango mkubwa wa
kuendeleza matumizi ya reli, Dar es Salaam umeandaliwa
na tumeanza kuutafutia fedha.
Usafiri wa Reli
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki tumetumia muda mwingi kutafuta
ufumbuzi wa matatizo yanayozikabili reli zetu za TAZARA
na TRC. Kimsingi reli hizo zimekuwa zinakabiliwa na
matatizo ya uchakavu wa miundombinu na uongozi na
uendeshaji usioridhisha. Kwa sababu ya matatizo hayo reli
hizi ambazo kila moja inaweza kusafirisha tani milioni 5
kwa mwaka zinasafirisha kati ya tani 200,000 na 300,000 tu.
65
Hivyo basi, mizigo mingi husafirishwa kwa barabara na
kutishia uhai wa barabara ambazo tumezijenga kwa
gharama kubwa.
Kwa upande wa reli ya kati, uboreshaji wa reli kati ya
Dar es Salaam na Tabora unakaribia kukamilika na
utaendelea mpaka Kigoma na Mwanza. Wakati huo huo
mchakato wa ujenzi wa reli mpya ya upana wa kimataifa
(standard gauge) unaendelea. Ujenzi unaweza kuanza
mwaka huu kutegemea kukamilika kwa majadiliano na
mabenki yaliyoonyesha utayari wa kutukopesha pesa za
ujenzi.
Mheshimiwa Spika;
Azma yetu ya kufufua reli ya TAZARA nayo
tumeiwekea mkakati. Sisi na Zambia tumekubaliana
kushirikiana kwa karibu katika kutafuta ufumbuzi wa
matatizo yanayoikabili reli yetu hiyo. Bahati nzuri marafiki
zetu wa China nao wamekubali kutusaidia katika mipango
yetu hiyo. Ni matumaini yangu kuwa safari hii tutapata
66
ufumbuzi wa kudumu kwa matatizo yanayoathiri ufanisi
wa reli hii yenye umuhimu wa aina yake kwa uhai na
ustawi wa uchumi wa nchi zetu na watu wake.
Bandari
Mheshimiwa Spika;
Tumeboresha na kuimarisha huduma katika bandari ya
Dar es Salaam kwa mafanikio makubwa. Mwaka 2014
bandari yetu ilihudumia tani milioni 14.4 ukilinganisha na
tani milioni 6.7 mwaka 2005. Mwaka huu inaweza kufikia
tani milioni 18. Siku hizi huduma hutolewa kwa saa 24 na
kasi ya kupakua, kupakia na kutoa mizigo imeongezeka
sana na wizi umepungua sana. Hata wale walioacha
kuitumia bandari yetu wameanza kurudi.
Mheshimiwa Spika;
Kuanza kutumika kwa mfumo wa Single Customs
Territory unaorahisisha upakuaji na upakiaji mizigo ya nchi
za Jumuiya ya Afrika Mashariki kumeongeza zaidi ufanisi.
67
Tuko katika majadiliano na DRC na Zambia ambao nao
wameonyesha nia ya kuingia katika mfumo huu.
Kuongezeka kwa usafirishaji wa mizigo inayopita
nchini kuna faida kwani sekta ya usafirishaji inachangia
zaidi ya asilimia 15 ya pato la taifa. Hali kadhalika, ujenzi
wa gati za 13 na 14 katika bandari ya Dar es Salaam
unaotegemewa kuanza mwezi huu utawezesha huduma ya
makasha kuongezeka kutoka makasha 600,000 hadi
makasha 1,200,000. Mipango ya kuboresha bandari za
Mtwara, Tanga na zile zilizo kwenye Maziwa yetu makuu
na ujenzi wa bandari ya Bagamoyo zitaiwezesha Tanzania
kunufaika na fursa ya jiografia yake.
Usafiri wa Anga
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki tumefanya jitihada kubwa ya
kuwekeza kwenye ukarabati, upanuzi na ujenzi wa viwanja
vya ndege nchini. Tumekarabati Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Mwalimu Nyerere ambao umeongeza uwezo
68
wa kuhudumia kutoka ndege 7 hadi 30 hivi sasa. Aidha
tunajenga jengo la tatu la abiria kwenye uwanja huo lenye
uwezo wa kuhudumia abiria milioni 3.5. Ujenzi huo
unategemewa kukamilika mwezi Oktoba mwaka huu.
Kukamilika kwake kutauwezesha uwanja wa Kimataifa wa
Julius Nyerere kuhudumia abiria milioni 6 na ndege nyingi
zikiwemo ndege kubwa za kisasa za Airbus 380.
Mheshimiwa Spika;
Vile vile, tumeufanyia ukarabati na upanuzi Uwanja
wa Kimataifa wa Kilimanjaro ambao ni muhimu sana kwa
sekta ya utalii ya ukanda wa kaskazini. Uwanja mpya wa
ndege wa Songwe kule Mbeya umekamilika na hivi sasa
unatumika. Hali kadhalika, tumeviboresha upya viwanja
vya ndege vya Arusha, Mafia, Mpanda, Kigoma, Tabora,
Mwanza na Bukoba.
Ujenzi, upanuzi na ukarabati huu tulioufanya,
umechangia sana katika ongezeko kubwa la safari za ndege
na abiria nchini. Safari za ndege kuja nchini zimeongezeka
69
toka safari 78 mwaka 2005 zilizokuwa zinatolewa na
kampuni 29 za usafiri wa ndege hadi safari 175 zinazotolewa
na kampuni 55 mwaka 2014. Aidha, abiria wanaoondoka na
kuwasili katika viwanja vya ndege wameongezeka kutoka
2,172,519 mwaka 2005 hadi abiria 4,670,380 mwaka 2013.
Siku hizi Watanzania wanaopanda ndege wanaongezeka
kwa kasi kubwa.
Mheshimiwa Spika;
Jambo ambalo hatukuweza kufanikiwa ni lile la
kufufua Shirika letu la Ndege. Tumefanikiwa kulifanya lisife
lakini hatukuweza kulihuisha lirejee hata kwenye ile hali
yake ya zamani. Hata hivyo, fikra na mawazo kuhusu
mkakati wa kulijenga upya shirika hilo yapo. Kwa sasa
Menejimenti imepewa jukumu la kuandaa mpango wa
biashara unaoeleweka na unaokopesheka, kisha Serikali
itaona namna ya kulisaidia shirika.
70
Utabiri wa Hali ya Hewa
Mheshimiwa Spika;
Sambamba na hayo, tumeboresha huduma za utabiri
wa hali ya hewa. Mamlaka ya Hali ya Hewa imepatiwa vifaa
vipya ambavyo vimeongeza ufanisi na usahihi wa utabiri
unaotolewa. Mwezi Februari 2014 Mamlaka hiyo ilipata
cheti cha utoaji wa huduma bora cha ISO na hivyo kuufanya
taarifa zake kutambuliwa kimataifa.
Mawasiliano
Mheshimiwa Spika;
Tumepiga hatua kubwa katika sekta ya teknolojia ya
habari na mawasiliano. Tumejenga Mkongo wa Taifa wa
Mawasiliano wenye urefu wa kilometa 7,560
unaounganisha miji mikuu ya mikoa yote ya Tanzania Bara
isipokuwa mkoa mpya wa Simiyu. Kwa Mikoa ya Unguja na
Pemba, ujenzi wake utakamilika mwezi ujao. Katika Awamu
ya Pili, Mkoa wa Simiyu na wilaya zote nchini
zitaunganishwa.
71
Ujenzi wa mkongo huu umechangia katika kuongeza
ubora na kasi ya mawasiliano, na kushusha gharama za
mawasiliano. Kwa mfano, gharama za kupiga simu
zimeshuka kutoka shilingi 115 kwa dakika mwaka 2005
hadi shilingi 34.92 mwaka 2014 na gharama za intaneti
zimeshuka kutoka wastani wa shilingi 36,000 kwa Gigabyte
moja mwaka 2005 hadi wastani wa shilingi 9,000 kwa
Gigabyte moja (GB 1) mwaka 2014. Hii imeshusha pia
gharama za biashara kwa kurahisisha mawasiliano na
malipo kati ya mabenki na kwa njia ya mtandao na simu.
Kwa upande wa laini za simu, zimeongezeka kutoka
laini milioni 2.96 mwaka 2005 hadi milioni 28 mwaka 2014.
Watu wanaotumia intaneti wameongezeka toka milioni 1.6
hadi milioni 9.3 mwaka 2014. Kukua kwa mawasilino ya
simu kumewezesha watumiaji milioni 12.3 kupata huduma
ya fedha kupitia simu za mkononi. Kati ya Julai 2013 na
Aprili 2014 jumla ya miamala milioni 972.6 ilifanyika yenye
thamani ya shilingi trilioni 28. Huu ni wastani wa zaidi ya
72
shilingi trilioni 2 kwa mwezi na kufanya Tanzania
kuongoza duniani kwa huduma hii.
Mheshimiwa Spika;
Tulitambua kuwa makampuni binafsi ya simu
hayapendi kuwekeza vijijini ambako biashara si kubwa
kama mijini. Kwa kutambua umuhimu wa huduma ya
mawasiliano kwa maendeleo, Serikali iliamua ibebe mzigo
huo. Kwa sababu hiyo tumeanzisha Mfuko wa Mawasiliano
kwa Wote (UCSAF) ambao utawezesha kata na vijiji vyote
nchini kufikiwa na huduma za mawasiliano. Mfuko huo
umekwisha wezesha jumla ya kata 52 na vijiji 314 kufikiwa
na huduma hizo. Upelekaji wa huduma za mawasiliano
kupitia Mfuko huo zinaendelea kwa kata nyingine 163 zenye
vijiji 922, ambapo wananchi milioni 1.2 watanufaika.
Mheshimiwa Spika;
Tumechukua hatua ya kuhakikisha kuwa mianya ya
kodi inazibwa na kwamba makampuni yanalipa kodi stahiki
kwa kununua na kufunga mtambo wa Kusimamia
73
Mawasiliano ya simu nchini. Mtambo huo unaowezesha
Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) kukusanya takwimu
halisi za mawasiliano yanayofanywa. Tangu kuanza
kutumika kwa mtambo huo, mwaka jana Serikali imeweza
kukusanya shilingi bilioni 24.6 ambazo vinginevyo
zisingepatikana. Aidha, tumekuwa nchi ya kwanza Afrika
ya Mashariki kuhama kutoka mfumo wa analojia kwenda
digitali. Karibu tutakamilisha kwa mikoa yote. Tunazipokea
nchi kadhaa zinazokuja kujifunza kwetu juu ya uendeshaji
wa zoezi hili.
Ardhi na Makazi
Mheshimiwa Spika;
Maisha bora kwa kila Mtanzania ni pamoja na
kuboresha makazi ya watu. Sote tunafahamu kuwa makazi
ni hitajio la msingi la binadamu. Lengo letu la kuboresha
huduma za ardhi, nyumba na makazi limepata mafanikio
makubwa. Tumepeleka huduma za utawala wa ardhi karibu
zaidi na wananchi kwa kuanzisha Kanda nane za
74
kusimamia upangaji, upimaji na utoaji hatimiliki. Uamuzi
huu umepunguza lile tatizo la watu kuchelewa kupata hati
miliki. Toka 2006 hadi sasa jumla ya hati 164,275
zimetolewa, vijiji 10,500 vimepimwa na kati yake vijiji 10,341
vimepatiwa hatimiliki.
Mheshimiwa Spika;
Tumetunga Sheria kwa ajili ya kuwezesha upatatikanaji
wa mikopo ya ujenzi na ununuzi wa nyumba. Sheria hizo ni
pamoja na Sheria ya Mikopo ya Nyumba (Mortage Finance)
na Sheria ya Kutambua Milki ya Sehemu ya jengo haswa
kwenye maghorofa (Unit Tittles Act) ya mwaka 2008. Sheria
hizi kwa ujumla wake zimewezesha watu wengi zaidi
kupata mikopo ya kujenga au kukarabati nyumba zao na
kuwawezesha watu kupata umiliki wa sehemu ya jengo.
Mabadiliko hayo pia yamewezesha sekta ya nyumba
kukua kwa kasi kubwa na majengo na nyumba za kisasa
kujengwa katika kipindi cha miaka 10 hii. Dar es Salaam ya
leo na ile ya 2005 ni tofauti kabisa. Shirika la Nyumba la
75
Taifa, Wakala wa Nyumba za Serikali, Mifuko ya Hifadhi ya
Jamii nayo imefanya uwekezaji mkubwa sana katika ujenzi
wa nyumba katika kipindi hiki.
Mheshimiwa Spika;
Kwa upande wa watumishi wa serikali kuwa na
nyumba mwaka 2008 tulianzisha Mfuko wa Mkopo kwa
watumishi wa umma ambao hadi sasa umetoa mikopo ya
shilingi bilioni 5.4 kwa watumishi 1,169. Pia, tumeanzisha
Kampuni ya Mikopo ya Nyumba kwa ajili ya watumishi wa
umma ambayo tayari imeanza kazi.
Mheshimiwa Spika;
Ninayo furaha kueleza kuwa makazi ya wananchi pia
yameendelea kuwa bora. Takwimu za Sensa ya Watu na
Makazi ya Mwaka 2012, inaonyesha kuwa idadi ya nyumba
zilizoezekwa kwa bati zimeongezeka kutoka asilimia 46
mwaka 2002 hadi asilimia 65 mwaka 2012. Kwa lugha
nyingine nyumba zilizoezekwa makuti na nyasi zimezidi
76
kupungua. Haya ni mafanikio makubwa ya kutia moyo na
hatua muhimu katika kuboresha maisha ya Watanzania.
Utafiti
Mheshimiwa Spika;
Jambo lingine ambalo tumeliwekea msingi mzuri ni
eneo la utafiti. Hili ndilo eneo ambalo ilitalivusha taifa letu
kwenda katika maendeleo makubwa zaidi. Niliamua
Serikali ichukue hatua za makusudi za kufufua shughuli za
utafiti ambazo zilikuwa zinapita katika kipindi kigumu.
Niliamua kuwa Serikali ianze safari ya kutenga fedha za
kutosha kwa ajili ya utafiti. Tulianza na shilingi bilioni 10
na kuendelea kuongeza mwaka hadi mwaka na kufika
shilingi bilioni 60 mwaka 2014, katika kipindi cha kujitahidi
kufikia asilimia 1 ya bajeti ya Serikali na hatimaye asilimia 1
ya pato la Taifa kwa ajili ya shughuli za utafiti.
Mheshimiwa Spika;
Kwa kutumia kiasi hiki kidogo kilichopo wanasayansi
wetu 344 wamepata ufadhili wa masomo ya shahada ya
77
Uzamili na 173 wa shahada ya Uzamivu. Miradi 70 ya
utafiti imefadhiliwa, kati ya hiyo 22 ni ya kilimo. Fedha hizi
pia zimewezesha Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia
kuanzisha viatamizi vya teknohama ambavyo vimewezesha
vijana wetu kubuni na kuvumbua teknolojia zenye manufaa
kwa maendeleo ya jamii na taifa. Wamezalisha ajira na
kunufaisha watu wengi. Kampuni ya Max Malipo ni mfano
mmojawapo mzuri wa matokeo mazuri ya viatamizi hivi.
Huduma za Jamii
Elimu
Mheshimiwa Spika;
Katika hotuba yangu ya kuzindua Bunge la Tisa
mwaka 2005 nilisema kuwa, Hakuna Taifa lililopata
maendeleo bila kuendeleza elimu. Hivyo kuendeleza elimu
nchini itakuwa agenda muhimu ya Serikali ya Awamu ya
Nne. Tumetimiza ahadi. Katika kipindi chote cha miaka
kumi bajeti ya sekta ya elimu ndiyo iliyokuwa kubwa kuliko
za sekta nyingine zote. Mwaka huu 2015 bajeti ya elimu
78
imefikia shilingi trilioni 3.4 ikilinganishwa na shilingi
bilioni 669.5 za mwaka 2005.
Mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya elimu ndani
ya miaka 10 hii ni ya kutia moyo. Tumeongeza shule za
msingi kutoka 14,257 mwaka 2005 hadi 16,538 mwaka 2015
na wanafunzi wameongezeka kutoka 7,541,208 hadi
8,202,892. Upanuzi huu umewezesha asilimia 98 ya watoto
wanostahili kupata elimu ya msingi sasa kuandikishwa.
Kwa kushirikiana na wananchi na sekta binafsi
tumeongeza Shule za Sekondari kutoka Shule 1,745 mwaka
2005 hadi Shule 4,753 mwaka 2015. Idadi ya wanafunzi
imeongezeka kutoka 524,325 mwaka 2005 hadi 1,804,056
mwaka 2015. Katika kipindi hiki pia vyuo vya Ufundi
vimeongezeka kutoka 184 mwaka 2005 hadi 744 mwaka
2015 na wanafunzi katika vyuo hivyo wameongezeka
kutoka 40,059 hadi 145,511 mwaka 2015. Haya ni mafanikio
makubwa sana.
79
Kwa nia ya kuongeza ubora wa elimu, tumechukua
hatua thabiti za kukabiliana na tatizo la uhaba wa walimu,
vitabu, maabara za sayansi na vifaa vya kujifunzia na
kufundishia. Tumepanua mafunzo ya ualimu wa Cheti,
Stashahada na Shahada. Hii imetuwezesha kuongeza idadi
ya walimu wa Shule za Msingi kutoka 135,013 mwaka 2005
hadi 202,752 mwaka 2015, na walimu wa Shule za Sekondari
kutoka 18,754 mwaka 2005 hadi 88,908 mwaka 2015. Uhaba
wa walimu wa masomo ya sanaa si tatizo tena, tunao wa
kutosha. Tuna upungufu wa walimu 20,141 wa masomo wa
sayansi na hisabati. Ninaamini, hata hivyo, kwa programu
za kusomesha walimu wa sayansi vyuoni zilizopo, katika
miaka michache ijayo tatizo hili nalo tutalipatia ufumbuzi.
Kwa mfano, Chuo Kikuu cha Dodoma, mwaka 2014
kimeanza kudahili wanafunzi 5,000 wa ualimu wa masomo
ya sayansi.
Mheshimiwa Spika;
80
Kwa upande wa maabara za sayansi, katika shule za
sekondari za kata tayari maabara 5,979 zimejengwa na
nyingine 4,410 ziko katika hatua mbalimbali za ukamilishaji.
Hivi sasa tunashughulikia upatikanaji na usambazaji wa
vifaa kwa matumizi ya maabara hizo. Kwa upande wa
vitabu tumeweza kuboresha upatikanaji wake kwa
mwanafunzi wa Shule za Msingi kutoka uwiano wa 1:5
mwaka 2005 hadi 1:3 mwaka 2015. Katika shule za sekondari
uwiano ni 1:2 ukilinganisha na 1:8 mwaka 2005.
Mheshimiwa Spika;
Katika kipindi hiki pia tumeshuhudia upanuzi
mkubwa wa elimu ya juu nchini. Idadi ya vyuo vikuu
imeongezeka kutoka vyuo 26 mwaka 2005 hadi 52 mwaka
2015. Miongoni mwa vyuo hivyo ni Chuo Kikuu cha
Dodoma na cha Nelson Mandela cha Arusha ambavyo
vimejengwa na Serikali ya Awamu ya Nne. Tumeanza
mchakato wa kujenga Chuo Kikuu cha Julius Nyerere cha
Kilimo kule Butiama. Vyuo hivi ni fahari ya nchi yetu kwani
81
tumevijenga kwa fedha zetu wenyewe bila msaada kutoka
kwa wafadhili. Ongezeko la vyuo vikuu limefanya idadi ya
wanafunzi kuongezeka kutoka wanafunzi 40,719 mwaka
2005 hadi 218,959 mwaka 2014. Idadi ya wanafunzi
wanaonufaika na mikopo nayo imeongezeka kutoka
wanafunzi 16,345 mwaka 2005 hadi wanafunzi 99,590
mwaka huu.
Afya
Mheshimiwa Spika;
Tumepata mafanikio ya kutia moyo kwa upande wa
kuboresha na kupanua huduma ya afya nchini. Tuliazimia
kusogeza huduma ya afya karibu na wanapoishi watu kwa
kujenga vituo vya kutoa huduma ya afya vipya na
kuimarisha vilivyopo. Kati ya mwaka 2005 na 2014 vituo vya
kutolea huduma za afya 2,175 vimejengwa. Kati yake
hospitali 19, vituo vya afya 168 na zahanati 1,883
zimejengwa.
82
Tumeimarisha hospitali ya Taifa ya Muhimbili,
Hospitali za Rufaa za Kanda, Mikoa na Wilaya kwa
kuzipatia vifaa vya tiba na uchunguzi (MRI, CT Scan, X ray,
Ultra Sounds, Maabara n.k). Tumejenga maabara ya Taifa ya
Afya ya Jamii ambayo inatumika kama maabara ya
Kimataifa ya Rufaa kwa nchi za SADC. Tumeimarisha
maabara za mikoa kwa majengo na vifaa vya kisasa vya
uchunguzi wa magonjwa. Maabara yetu ya Mbeya sasa ina
uwezo wa kubaini virusi vya Ebola jambo ambalo miezi
michache iliyopita tulikuwa tunapeleka sampuli Nairobi.
Hivi sasa hospitali za wilaya zinaweza kufanya uchunguzi
wa mwenendo wa figo na ini.
Mheshimiwa Spika;
Tumeboresha huduma ya Afya ya Kinywa katika
Hospitali ya Muhimbili kwa kufunga mashine 26 za kisasa
za tiba ya meno na maabara ya kisasa ya kutengeneza meno
bandia. Pia tumeimarisha huduma ya afya ya kinywa kwa
kuweka vifaa vya tiba ya meno kwenye Halmashuri 91. Hivi
83
sasa hospitali 136, vituo vya afya 63 na zahanati 3 zinatoa
huduma hiyo nchini.
Tumeanza kupata mafanikio katika dhamira yetu ya
kujenga uwezo wetu wa ndani wa kuchunguza na kutibu
maradhi ya figo, moyo, saratani na mishipa ya fahamu
ambayo tumekuwa tunapeleka wagonjwa wengi nje. Kwa
mfano, tangu Taasisi ya Moyo ianze kutoa huduma pale
Muhimbili wagonjwa 71,963 wamepatiwa matibabu
wakiwemo 692 waliofanyiwa upasuaji. Watu hao
wangepelekwa nje taifa lingelipa pesa nyingi. Uwezo wetu
utaongezeka sana hospitali ya Mloganzila itakapokamilika.
Mheshimiwa Spika;
Tumebadilisha utaratibu wa kusambaza dawa kutoka
Bohari ya Dawa. Tumeongeza bajeti ya dawa na vifaa tiba
kutoka shilingi bilioni 40.6 mwaka 2005 hadi shilingi
bilioni 147 mwaka 2014. Idadi ya watu wanaonufaika na
Mfuko wa Afya ya Jamii na Mfuko wa Bima ya Afya
84
wameongezeka kutoka asilimia 3 mwaka 2005 hadi asilimia
19 mwaka 2014.
Katika kipindi hiki tumetoa msukumo mkubwa katika
kupambana na maradhi makubwa ya kuambukiza
yanayosababisha vifo vya watu wengi. Tumeendesha
kampeni ya kupambana na malaria nchi nzima kwa
kubadilisha dawa ya kutibu malaria na kugawa vyandarua
26,371329 kwa watoto chini ya miaka mitano, kwa akina
mama wajawazito na katika kila kaya. Aidha, tumepulizia
dawa ya kuua mbu ndani ya nyumba katika mikoa ya kanda
ya ziwa. Matokeo ya jitihada hizo ni kupungua kwa
maambukizi ya malaria kwa asilimia 51 na vifo kwa
asilimia 71. Baada ya kiwanda cha kuzalisha dawa ya kuua
viluwiluwi vya mbu pale Kibaha kuanza uzalishaji, safari ya
kutokomeza malaria hapa nchini ni ya uhakika.
Mheshimiwa Spika;
Juhudi zetu katika kupambana na ukimwi
zimewezesha kushuka kwa maambukizi ya ukimwi kutoka
85
asilimia 7.7 mwaka 2005 hadi asilimia 5.1 mwaka 2012.
Idadi ya watu waliopima virusi vya ukimwi imeongezeka
kutoka 365,189 mwaka 2005 hadi 25,468,564 mwaka 2014.
Aidha, tumewezesha vituo 5,244 na asilimia 97 ya vituo
vyote vinavyotoa huduma ya uzazi kutoa huduma ya kuzia
maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.
Mheshimiwa Spika;
Kati ya mwaka 2005 na 2014 tumeongeza udahili wa
wanafunzi katika vyuo vya afya kutoka 3,025 mwaka 2005
hadi 11,807 mwaka 2014. Katika kipindi hicho wataalamu
wa afya 55,608 wameajiriwa. Aidha, tumeongeza ajira ya
kada mbalimbali za afya. Kwa sababu hiyo idadi ya
madaktari imeongezeka kutoka madaktari 1,048 mwaka
2006 hadi madaktari 2,325 mwaka 2014. Halikadhalika,
madaktari wasaidizi wameongezeka kutoka 1,223 hadi
1,914, wauguzi kutoka 15,961 hadi 22,942 wataalamu wa
Maabara kutoka 1,277 hadi 2,378 mwaka 2014. Hivi sasa
uwiano wa Daktari kwa wagonjwa ni 1:6,666 ikilinganishwa
86
na 1:35,714 mwaka 2005. Na, uwiano wa Muuguzi kwa
wagonjwa umeshuka kutoka 1:2,347 mwaka 2005 hadi
1:2,008 mwaka huu.
Mheshimiwa Spika;
Tumeendesha kampeni ya kuboresha lishe nchini na
kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Lishe (2011-2016). Kwa ajili
hiyo mwaka 2013 tulizindua Programu ya Uongezaji wa
Virutubishi. Matokeo ya jitihada zetu hizo yameanza
kuonekana. Udumavu umepungua toka asilimia 44 mwaka
2005 hadi asilimia 35 mwaka 2014 na uzito pungufu toka
asilimia 17 hadi asilimia 13.
Kwa jumla juhudi zetu za kuboresha huduma ya afya
zimezaa matunda ya kuridhisha. Wastani wa umri wa
kuishi wa Mtanzania umeongezeka toka miaka 49 mwaka
2005 hadi miaka 62 hivi sasa. Vifo vya watoto wachanga
vimepungua toka vifo 68 kwa kila vizazi hai 1000 hadi vifo
21 kwa kila vizazi hai 1,000 mwaka 2014. Vifo vya watoto
chini ya miaka mitano vimepungua kutoka vifo 112 kwa kila
87
vizazi hai 1000 mwaka 2005 hadi vifo 54 kwa kila vizazi hai
1000 mwaka 2014, na vifo vya akinamama wajawazito
vimepungua toka vifo 578 kwa vizazi hai 100,000 hadi vifo
432 kwa vizazi hai 100,000 mwaka 2012. Haya ni mafanikio
ya kutia moyo ingawaje bado tunatakiwa kuendeleza juhudi
zaidi mara dufu ili vifo vipungue zaidi na zaidi.
Maji
Mheshimiwa Spika;
Serikali ya Awamu ya Nne imefanya juhudi kubwa
katika kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji safi na
salama na usafi wa mazingira katika kipindi hiki.
Tumekamilisha miradi ya maji katika miji mikuu ya mikoa
8, Wilaya 6 na Miji midogo 2. Aidha, miradi katika miji
mingine 13 ya mikoa, 27 ya Wilaya na Miji midogo
inaendelea kutekelezwa. Utekelezaji wa miradi hii
umewezesha kiwango cha upatikanaji maji mijini kufikia
wastani wa asilimia 86 kwa mwaka 2014 kutoka asilimia
73 mwaka 2005. Na kwa Vijijini imefikia asilimia 67.6
88
Mwaka 2014 ukilinganisha na asilimia 53 mwaka 2005.
Tumevuka lengo letu la kuwapatia maji asilimia 65 ya
wakazi wa vijijini.
Aidha, miradi inayoendelea kutekelezwa hivi sasa
itakapokamilika katika mwaka huu wa fedha upatikanaji wa
maji mijini utafikia asilimia 90 ambalo ndilo lengo la Ilani ya
uchaguzi ya CCM. Vijijini inaweza kufikia asilimia 70
ambayo ni juu ya lengo la asilimia 65.
Aidha, tumeboresha huduma za uondoaji wa maji taka
katika miji ya Tanga, Dodoma, Mwanza, Mbeya, Iringa,
Songea, Tabora na Morogoro. Uboreshaji huu wa huduma
za utoaji wa maji taka ni mwanzo mzuri katika kuhakikisha
kwamba tunakuwa na mipango mizuri ya maji taka mijini.
Uwezeshaji wa Wananchi
Mheshimiwa Spika;
Uwezeshaji wa wananchi kiuchumi ilikuwa ni moja ya
dhima kuu ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005.
Katika kutekeleza dhamira hii, Serikali imeendeleza kwa
89
mafanikio makubwa mifuko ya kutoa mikopo kwa vijana,
wanawake, wajasiriamali wadogo na kuanzisha fursa
nyingine mpya. Watu wengi wamenufaika na wao wenyewe
kuwa chachu ya kuzalisha ajira, kupunguza umasikini na
kuinua hali za maisha ya watu walioguswa na fursa
zilizopatikana.
Tumeiwezesha Benki ya Wanawake kuanza na
kuendelea kutoa huduma. Kama mjuavyo niliamua Serikali
ichangie mtaji wa mwanzo na inaendelea kuchangia mtaji
huo. Tayari Benki hiyo imeshakopesha watu 125,000 na kati
yao wanawake ni asilimia 82. Hali kadhalika, nilifanya
uamuzi wa makusudi wa kuifufua Benki ya Rasilimali (TIB).
Dhamira yangu ni kutaka iwepo Benki ya maendeleo
itakayotoa mikopo ya muda mrefu na wa kati kwa
wawekezaji wazawa. Hii itawezesha kuanzisha na
kuendesha shughuli za viwanda, madini, utalii na biashara
kwa urahisi.
90
Tumeiwezesha Benki ya Rasilimali kwa mtaji, rasilimali
watu na vitendea kazi na kuifanya iwe moja ya benki ya
kutumainiwa nchini. TIB imeshatoa mikopo kwa
makampuni 365 yenye thamani ya shilingi bilioni 512.
Aidha, imetoa mikopo kwa miradi 201 yenye thamani ya
shilingi bilioni 156 kupitia dirisha dogo la kilimo. Natoa
pongezi maalum kwa viongozi na watumishi wa Benki ya
Rasilimali kwa kazi kubwa na nzuri waliyofanya katika
kipindi hiki kifupi. Naomba waendelee na moyo huo kwa
maslahi ya nchi yetu.
Mheshimiwa Spika;
Tumetimiza ahadi yetu ya kuimarisha ushirika nchini
kama nguzo kuu ya kuunganisha nguvu za wanyonge
kujiletea maendeleo. Katika kipindi hiki, idadi ya Vyama
vya Ushirika vya aina mbalimbali nchini imeongezeka
kutoka 5,832 mwaka 2005 hadi 9,604 mwaka 2015.
Kwa upande mwingine, Vyama vya Akiba na Mikopo
(SACCOS), vimeongezeka zaidi ya mara tatu kutoka vyama
91
1,875 mwaka 2005 hadi 5,559 mwaka 2014. Akiba, hisa na
amana za wanachama zimeongezeka kwa zaidi ya mara
tano kutoka Shilingi bilioni 85.6 mwaka 2005/2016 hadi
Shilingi 463 bilioni mwaka 2014 na mikopo kwa
wanachama imekua mara 13 toka shilingi bilioni 65.7 hadi
shilingi bilioni 893 mwaka huu. Kwa hakika haya ni
mafanikio makubwa ya kujivunia. Watu wengi
wamewezeshwa kupunguza umasikini wao na wengine
kuondoka katika lindi la umasikini.
Sanaa na Michezo
Mheshimiwa Spika;
Niliahidi kusaidia kukuza michezo na sanaa nchini.
Kwa upande wa michezo niliahidi kuwa Serikali italipia
makocha. Nilitimiza ahadi yangu kwa michezo ya soka,
netiboli na ngumi. Kwa upande wa riadha tuliwapeleka
wanariadha wetu China, Ethiopia na New Zealand kwa
maandalizi ya mashindano ya kimataifa. Timu yetu ya taifa
ya soka haijafanya vizuri sana. Kwa upande wa soka
92
tulianza kupata matumaini lakini baadae yakafifia. Timu
yetu ya taifa ya soka haijafanya vizuri sana pamoja na
kubadili makocha. Hata vilabu vyetu pia havifanyi vizuri.
Kwa kweli lazima Watanzania tukae chini na kujiuliza kwa
nini hatufa